The Chant of Savant

Wednesday 21 January 2009

Niliwaonya kuhusu Kagodamn

Kikundi Abtari na Gendaeka, Ogofyo na Dumuzi Angamizi au Kausha, Goma na Danganya kijifichacho nyuma ya ukuu na wakuu; ni kampuni lililoundwa na mbweha na vyangudoa wa kisiasa kuwahonga walevi ili waukwae mkenge baada ya kufakamia takrima na hongo kila aina.
Hawa jamaa ni rafiki zangu wa damu. Ajabu eti walevi walitaka niwakaange wasijue sote dugu moja. Ingawa fisi anasifika kwa uchoyo na ulafu, hawezi kumla wenzake wakati aongoza kundi la kondoo. Nani mpumbavu aukate mkono unaomlisha?
Mimi siyo kama yule shehe ubwabwa atabirie uongo ili apewe njuluku. Nilitabiri na kutabiri kuwa Kagoda na Richmonduli ni vitendawili ambavyo hakuna mteguzi atavitegua akawa salama. Nilionya mara si moja. Hakuna upumbavu kama kutegemea mkulima ashinde kesi yake inapokuwa mikononi mwa ngedere. Nilionya: haiba zetu zinawadanganya wengi. Tupo wengi majambazi lakini huwezi kututambua kutokana na majoho tuliyovaa. Mnashangaa nini mlevi kuwa shehe au shehe kuwa mlevi? Hakuna uzembe kama kumwachia nguruwe kitani cheupe akifue ukategemea kitatakata. Kwani kazi ya mchwa nini hata kama kanenepa? Muweke mchwa kwenye bunda la makaratasi utalia wewe na kuonekana juha. Kwani hamkuonywa?
Kinachonikera ni ile hali ya walevi kuchangamkia mvinyo ule ule baada ya kubadilishiwa chupa! Tena mvinyo uliochanganywa na mikojo kwenye maabara ya mlevi! Kwani hamkujua? Mbona mzee wa Kuchonga alionya na kuonya msimuelewe? Mlitegemea nini kama wafuasi wake walimfanyia kile Yuda Iskarioti alichomfanyia mwana wa Adam?
Basi waliwa na wanyonywa msijihangaishe kuwatafuta Kagoda. Jamaa wanaishi mtaa wa pili wakiwafadhili wakubwa na wadogo. Mambo yaliharibika mlipouza ukuu ukaanza kupatikana kwa hongo na ukubwa wa fuko la mwizi. Kumbe hamkujua jamani?
Hamkujua kuwa Kagodamn wana nguvu za ajabu! Mtu alambe madafu milioni arobaini halafu makapuku wamsurubu! Thubutu. Atahonga hata wale msiowategemea. Ila huyu hakuhonga bali alitumiwa na wale mliowaamini na kuwategemea msijue mbwa ni mbwa. Mliishaambiwa penye udhia penyeza rupia. Mambo yalianza zama zile kabla ya abracadabra kutembezwa. Na kwa taarifa yenu hii ndiyo siri ya Tunituni kujikalia kimya akijua wazi atakayemgusa naye atamuumbua. Yeye si mpumbavu ingawa ni mpuuzi. Alifanya mambo akijua hatima yake.
Unakwenda pale Brelia unachomoa nyaraka mambo kwisha. Unawadedisha akina Balalii na kuona nani mwenye ubavu wa kukufichua.
Mlionywa patakatifu pa patakatifu siyo sehemu ya wabadili pesa na wasasi wa ngawira hamkung’amua. Sasa yamewakuta mnaanza kulalama!
Hivi jamani nani aliwaroga nyie walevi kujiona mwajua kuliko mzee Musa hata kama alikuwa bingwa wa kuchonga? Nani aliwaroga nyie kudhani kuwa Mpayukaji anaweza kuwatosa washhirika zake akina Mbwadogi?
Kama mnawataka akina Kagoda basi mwambie mkuu wenu aje nimpe orodha na jinsi mchezo ulivyochezwa. Mwambie aje tuongee vizuri na ahakikishe usalama wangu muone kama sitawataja. Ningewataja hata leo. Lakini nami ni binadamu naongopa kukolimbwa na kubaliliwa au kuambiwa mimi si raia bwana. Nitaelezaje iwapo jamaa haaminiki. Anasema hili anatenda lile. Siwezi kufanya uzembe huu kumwamini kama nyinyi mlivyofanya msijue mtajuta. Ajabu mtazidi kudanganywa na ikifika taimu ya kufanya kweli mtaletewa mikagoda mingine.
Msingekuwa mafisadi wa kimawazo mliozaliwa na mama yenu woga na kulalama ningewataja potelea mbali liwalo na liwe.
Kwa vile utabiri wangu huwa siyo kama wa shehe Yoyo wa Ubwabwa, natabiri balaa jingine. Huko tuendako jamaa zangu akina Rambaramba na son of Jona wa Upare watapeta na kulipwa njuluku zenu mbaki vinywa wazi mkilalama kama mainzi mafu kwenye mzoga yatimuliwapo na mbwa.
Mlizidiwa kete pale jamaa alipoonyesha uchungu na madafu milioni milioni 12 huku akiwaandaa kisaikolojia kuzika milioni milioni 40 za Kagodamn. Wajinga ndio waliwao. Badala ya kuhoji mlimwagia sifa msijue alikuwa akiwakaanga samaki kwa mafuta yao ukiachia mbali kuwaandalia kiama cha Kagoda kupeta kama hana akili nzuri.
Asubuhi niliongea na mwanzilishi wa Kagoda Rost Tamu L’Aziz akanizodoa kuwa yako wapi sasa. Kabla ya kumpaka nilipokea simu toka kwa Malengesi mwezeshaji mkuu wa Kagodamn aliyenionya niache kujitia tia!
Ila niliwaambia kuwa siku ulevi ukiwatoka walevi yanayotokea kwa Bob Mugabe yanaweza kujiri kayani.
Huwezi kuamini kuwa majambazi hawa wawili walinitia hasira nikaenda hadi kujaribu kuingia sehemu sehemu au patakatifu pa patakatifu ili nimrambe vibao Chekacheka. Utaamini nikikwambia kuwa wakati natia timu langoni niliona magari ya Rost Tamu na Malengesi, Ewassa, Enderea Chenga. Joe Makambako na majambazi wengine wakiingia kuangusha party ya kujipongeza. Hata yule Fenesi aliyetumiwa kutoa habari mbaya alikuwapo akichekacheka na kujiona mjanja asijue hatima ya vitegemezi tumeiweka pabaya.
Nilikuta walinzi wakihoji inakuwaje makabrasha yanayotunzwa na watu wanaolipwa mishahara tena wakajulikana yapotee hivi hivi. Mmoja wao inaonekana anawajua walevi na wagema wao. Alijibu hoja hii kwa swali. “Nani mkuu wa hiyo Brelia?” alijibiwa mdogo wake Tunituni aitwaye Ben.
Naye akamalizia. “Nani alitegemea mbweha amuumbue fisi wakati wote ni hayawani wapenda nyama ukiachia mbali kuwa ukoo mmoja?
Hakuna kosa kama kuwachia paka maziwa au ngedere mahindi halafu akafanya kweli ukaanza kujiliza na kulaumu. Yametokea ya Kogodamn. Kwani kesho kutwa ni mbali ambapo kila mmoja atakuja mbele ya baraza kujigonga ili apewe ulaji? Je walevi wana kumbukumbu na ithibati ya kufanya kweli kama pale kwa Nyayo hata kama nako kumeishia kuwa yale yale?
Hakuna dhambi kubwa kama kulalama wakati uwezo wa kuondoa kwa mkono upo. Sasa mmetiwa madole machoni. Tutaona mtafanya nini kuonyesha kuwa nyie si mazezeta mateka wa wezi wale washirikianao tena kwa kutumia madafu yenu wenyewe na kila kitu chenu kuwaumizeni.
Kile kizee chenye jina kama Kamba kiliposema EPA ilikuwa imeisha kilikuwa kikijua kinachosema. Kilikuwa kikiwaweka sawa tayari kwa kupokea fumbo la imani Kagoda hakamatiki, Kagoda amepotea, Kagoda yumo miongoni mwenu. Kagoda ni mkuu kwenu. Kagoda ni mwajiri wenu na Kagoda ni yote katika yote.
Hekima ya leo. Maiti ni maiti hata avishwe suti na kutonwa madini ya thamani. Je mpo? Tieni akili mjikumbushe maonyo yam zee Musa wa Kuchonga aliyelala kule Buti Ama! Ila kilicho na mwanzo….malizia. Tuliwaona akina Mabutu na Bokassa. Wamezikwa kama mbwa kusiri tena aso mwenyewe.
Chanzo: Tanzania Daima Januari 21, 2009.

No comments: