The Chant of Savant

Wednesday 23 June 2010

Kiherehere cha vibinti, vibaba au watuwala?

MASAAMU Masaamu daktari daktari
Masamu wajile tutakuroreninde?

Masamu y’ egetonto
Muntu musaja muntu mukungu
Ni kiwe we niki musubati niki mukungu?

Omonene tataaa ehee
Tindi kuzurate x 2.

Huu ni wimbo mzuri lakini wa kilugha, acha niimbe wa Kiswahili. Mura Alex Msama upo hapo?

Kiherehere wee kiherehere wee
Wanafunzi acha kiherehere
Wanasiasa acha kiherehere
Walimu nanyi acha kiherehere
Maprofesa acha kiherehere
Siri-kali ache kiherehere
Rai… wee acha kiherehere
Wauza chips acha kiherehere weee kiherehere wee
Umeogelea kwenye mwamba? Eee
sorry sana.


Baada ya rafiki yangu mkuu kupata ugonjwa kama wangu (kupayuka) akapayuka, nilijikuta nikikumbuka huu wimbo tuliozoea kuuimba kipindi fulani mambo yalipo kuwa si mambo. Uzee mwingine unaanza vibaya hasa ukichanganyikana na ulevi wa maulaji.

Siku moja nilimuimbia shangingi mmoja wa kinshomile aitwaye Silvia Rweyependekeza wimbo huu nusu aninyotoe roho. Hayo tuyaache.

Si juzi tu bwana Nkubwa alipopatwa na kashfa ya kuvitukana vishikaji-sorry vibinti vyake kuwa vinadungwa mimba na wakwale wa kiume kwa vile vina kiherehere! Waliouliza yeye anaumwa ugonjwa gani kama si kiherehere hadi awapayukie wafanywa kazi na siku chache baadaye awakashfu wanafunzi?

Je, huyu hajampa mtaji yule mwalimu wa kisukusi anayeoa madenti wake ukiachia mbali wale wanafunzi wanaodunga mimba wenzao na kuwalaza mahospitalini wakati wao wanakula book?

Hebu ninukuu msidhani umbea. “kila anayepata ukimwi anautafuta mwenyewe na wengine ni viherehere vyao; kwa mfano watoto wa shule.” !!!!!!!!!!!!!. Mwanawitu!! Kama huu ndiyo msimamo wa mkuu tumeliwa na tumekwisha.

Mbona kama wao si viherehere wanaogopa kupima ukimwi achia mbali ukiwanyotoa wanavyosingizia mashinikizo ya blood?

Kwanza, kama mzazi siwezi kupata ubavu wa kupayuka hivi hata kama nina ugonjwa huu. Sina ubavu wala hicho kiherehere kuyatamka makufuru haya kusema ule ukweli.

Pia ukiangalia umbali toka Ng’wanza alipoyatamkia na Kishapu na kwingineko kwa akina chagulaga, ni kama ametoa baraka kuwa sasa vibinti vyetu vitolewe kafara hasa na wale wazazi wanaoabudia ng’ombe na fweza.

Japo tunalaani ukeketaji wa viungo, huu wa kiakili ni hatari zaidi hasa unapoungwa mkono na mkuu mwenyewe.

Badala ya kuamuru wanaodunga mimba vitoto vya shule wachapwe bakora na kufungwa, mnawachapa bakora walimu! Ama kweli hii ndiyo Kanani yenyewe ya waharifu na mafisadi!

Sitaki nionekane namshambulia mkuu hata kama tuna ugomvi wa kisiasa. Alichosema waarabu huitaa sharaabiin al nukhama tafsiri sitoi.

Leo najikumbusha enzi zangu nikifundisha kwenye chuo kikuu cha Havard. Zama zile Ziro alikuwa mwanafunzi wangu. Hivyo nitatoa lecture kuonyesha kuwa mimba mashuleni si kiherehere cha wanafunzi bali wanasiasa.

Hivi unategemea nini unapofanya maisha ya wanakaya kuwa magumu kwa kuruhusu mfumko holela wa bei huku ukitanua majuu kwa njuluku hiyo hiyo?

Je, kupenda mialiko pekee si kiherehere kinachosumbua wana siasia wetu? Je kupenda ‘per diem’ ambazo hupatikana kwa kuhudhuria washa, semina na makongamano ya ulaji si kiherehere kingine?

Je, serikali kuridhia nyumba za kufanyia ngono chapu chapu au maarufu kama guest houses zisizo na wageni si kiherehere? Hebu jikumbushe nionayo mtaani kwangu pale Tabata Liwiti. Kila kona ni grosari na kibanda cha chips. Ajabu upuuzi huu umezunguka kila shule na kila sehemu hata misikiti na makanisa. Je, kiherehere cha kisera kama hiki si balaa la wanyonge mkuu?

Kaya yenye sera kama hizi haikosi kihorohoro cha maisha kiasi cha watu kujiuza hasa pale nchi inapouzwa kwa wachukuaji waitwao wawekezaji.

Huyu anauza madini, yule mkoa wake na wengine hata miili yao. Wakati hawa wakiwa na kiherehere cha kupayuka wale wana cha kuuza miili yao na wengine kughushi hata vyeti vya kitaaluma na kuzaliwa mradi kila mtu anakula kwa kiherehere chake.

Hapa hujagusia kiherehere mama wa viherehere, yaani ufisadi wa kuhongana kitochi hadi mnaibiana kula ya kura katika uchafuzi ujao kwa uchaguzi.

Je, kutowashughulikia kina Kagoda and your company si kiherehere ukiachia mbali kuiba majumba ya kaya? Kwanini hii kaya isiwe ya viherehere kiasi cha kushindwa kujua ni kiherehere gani anamsema gani?

Kuna ukweli katika hili. Kweli wanafunzi si viherehere hasa wale wanaochangia wanasiasa wakati sera zao zinawabinya wao?

Nenda pale Udom kaulize juzi walifanya nini kwa kumchangia nani wakati nijuavyo kama profesa mzoefu maisha ya vyuoni ni ya dhiki sana. Ajabu ya maajabu ni pale maji yanapokimbia toka jangwani kwenda baharini! Siasa na elimu wapi na wapi?

Nenda pale Mabibo Hostel hata Milimani complex ujue kuwa viherehere si wasichana tu bali hata wababa watu wazima na heshima zao.

Kabla ya kampeni za mwaka 2005 kuna kiherehere mmoja namjua alikuwa akienda pale Mlimani kutafuta wasichana viherehere wa kufanya kiherehere chake nao.

Tujiulize kwanini vibinti vyetu vimekuwa na kiherehere. Je, ni cha kurithi au kuambukizwa nasi wazazi viherehere wa kila kitu kuanzia siasa hadi maadili na madili?

Hivi wazazi wanaozaa hovyo hovyo nje ya ndoa si viherehere? Nani mara hii amemsahau yule mheshimiwa toka Zenj alokuwa kaoa mwanafunzi na serikali haikumchukulia hatua?

Hata ukienda kwenye vyuo vikubwa, utakuta walimu wakiwataka wanafunzi wa kike ngono lau wawape hizi shahada za mavazi ya ndani. Lisirikali limefanya nini kuwabaini hawa na kuwatimua hata kuwafunga? Ajabu hata ajira nono nono serikalini hata siasani siku hizi zina dalili za kamchezo haka.

Najua wabaya wangu watapakaza kuwa nampakazia jamaa kwa sababu nimepania kuingia ikulu mwaka huu. No. Kwanza mimi ni mzazi ninayeheshimika sana hom kwangu na nina mabinti wengi. Pili, nimeokoka baada ya kuwa na ugonjwa wa kiherehere kiasi cha kuwa na nyumba ndogo kila mtaa ukiachia mbali idadi ya watoto wangu kushindana na swahiba yangu Jacob Zuma ambaye bi mkubwa wake ameamua kurivenji siku zilizopita kiasi cha kuiacha dunia kinywa wazi. Zuma akifanya kiherehere ruksa. Lakini Nompumelelo akijibu mapigo kwa kiherehere hiki nongwa siyo?

Hakuna kitu kimenistua na kunifurahisha kama kufichuka kwa usanii wa shirika moja la kikubwa lenye kujidai linatetea vitoto vya kike na akina mama la MAWAWA.

Baada ya daddy kupayuka na kuchafua hewa ajabu halikujitokeza kumpinga lau kwa upole! Huu ni ushahidi kuwa MAWAWA ipo kutafuta mtaji kifedha na kisiasa kwa kuwahadaa walengwa nao waingie kiherehere chake cha kutafuta ngawira.
Chanzo: Tanzania Daima Juni 23, 2010.

No comments: