The Chant of Savant

Friday 15 October 2010

Matokeo ya utafiti wa KEDET kuelekea uchaguzi

















Dk. Longolongoson Bunner (msomi nepi na nyemelezi) akitoa matokeo ya utafiti wa uongo na kifisadi uliodhaminiwa na Chama Cha Mafisadi (CCM)



BAADA ya Redet kutoa matokeo ya utafiti juu ya maoni ya walevi kuelekea uchakachuaji matokeo na kubebana, na Kijiwe kimetoka na matokeo yake chini ya asasi yake isiyo na makengeza wala upendeleo ya Kedet yaani Kijiwe Electoral and Democratic Evaluation Trust.

Wakati Redet ilihoji watu wao wasiofikia hata 3,000, Kidet imehoji walevi karibu wote kaya nzima. Katika utafiti huu walevi wameonyesha wazi kumchukia mtu mmoja aitwaye Njaa Kaya na Chama Chake Cha Maulaji.

Kidet ilitoa dondoo zifuatazo kwenye hoja zake.

Mwaka huu utamchagua nani na kwanini? Asilimia 80 ya waliohojiwa wanasema watamchagua Dokta Silaha na sababu waliyotoa ni kumlipizia kisasi Njaa Kaya kwa kuwaahidi Kanani akaishia kuwaswaga motoni huku Kanani ikijaa mafisidi na mafisi.

Pili, je serikali iliyomaliza muda wake imekidhi matarajio yako na kuna haja ya kuipa ridhaa tena?

Asilimia 90 ya waliohojiwa wametoa majibu yenye kila aina ya ukweli na kulipiza kisasi.

Tutanukuu majibu ya mmoja wa walio hojiwa aliyeandika kama ifuatavyo: “Tulitoa kura tupate maendeleo na maisha bora. Sasa tunahangaika na kuendelea katika kutoendelea huku maisha yakiwa maisha balaa badala ya maisha bora! Tumo msambweni tukilalama na kutumiwa kama wanyama wa mizigo-beasts of burdens! This should not be repeated.”

Tofauti na Redet, Kedet siyo NGO ya ulaji wala kujikomba kwa yeyote.

Chini ya wakurugenzi wa Kedet, Profesa Mpayukaji Msemambovu na Dk. Msomi Mkatatamaa, yafuatayo ndiyo matokeo ya utafiti uliohusisha walevi, vibaka, wachumia tumbo na wajigongaji-bootlickers and cheerleaders and praise singers.

Hawa tumewapata kwenye mabaa, madanguro, vijiwe vya kahawa na vya kuuzia bangi na gongo. Kwa upande wa wanasiasa na wachumia tumbo tuliwapata kwenye mikutano ya kampeni na uchakachuaji ukiachia mbali kwenye lisirikali la Njaa Kaya mwenyewe.

Wajumbe wa kamati ya Kedet walitolewa mkuku maeneo ya wazito kwa kupigiwa zegere la mwizi huku walinzi na mbwa wa getini wakitoa mpya kwa kutishia kuwanyotoa roho wadodosaji wetu.

Kidet ilizunguka Kaya nzima kwa mtaji wa pesa ya kahawa na kuibuka na yafuatayo.

Kwanza, wanakaya waliokuwa wakimmwagia ujiko Mkuu wanaonekana kubadilika vilivyo. Wanasema wazi kuwa amewaangusha na kuwasaliti. Utafiti unaonyesha kuwa kiwango cha kuungwa mkono na kuaminiwa kimeshuka kutoka asilimia 89 hadi 19.

Katika nyanja ya kukidhi matarajio na kuaminika katika ahadi zake, Mkuu ameibuka na asilimia 11. Asilimia hizi amezipata kutokana na kuweza kuunganisha nyumba zake na marafiki kwenye ulaji wake.

Ukilinganisha na asilimia nyingi alizokuwa alipoukwaa baada ya walevi kuukwaa mkenge, ni kwamba Mkuu ametoka kapa kwenye uongozi bora. Amefanikiwa kwenye uongo bora ulioweza kuwafanya wananchi wasiingie mitaani baada ya kuangusha vibaya sana.

Kwenye uwajibikaji ameambulia asilimia tano au kutoka kavu kabisa. Hata hizi asilimia tano amezizoea kutokana na kuwajibika kwa marafiki na familia yake.

Kwenye kipengee cha maendeleo, Mkuu ameendelea sana kuanguka kutokana na kuelekeza maendeleo kwenye jamaa zake na chama chake huku wanakaya wakikosa maendeleo kabisa. Kitaalamu amepata asilimia zinazotafsirika kama HOVYO. Yaani Hakuna organizasheni, visheni yeyote na open policy. Uchumi umezidi kuendelea katika kifo cha kuporomoka na kutegemea takwimu za wajanja fulani.

Kwenye eneo la mipango, Mkuu amepata alama tisa ambazo kitaalamu zinatafsiriwa kama CHOVU yaani Choka mbaya, hali holelea, ovyo, vurumai kiutawala na ufisadi.

Kutengeneza ajira, Mkuu amepata alama maarufuku kama CHOO yaani Chakavu, hasara, ovyo na omba omba.

Tahadhari. Msomaji inabidi uvumilie kupambana na maneno-terminologies ngumu kutokana na hali halisi ya mambo ambapo kwa miaka mitano mafanikio yaliyotokea ni hasi. Mfano, kumekuwa na mafanikio kwa kundi dogo la wanasiasa na wasaka ngawira wengine ambao wamefanikiwa kuzidisha utajiri wao na kukuza mazingira ya kuiibia Kaya kama vile kusaini mikataba mingine feki huku ikiundwa tume ya ulaji kwa nia ya kuwazuga wanakaya na kuwachanganya wapingaji. Rejea kutaka kunyakuliwa kwa Kabwela ambaye chama chake kimeonyesha ukomavu kwa kuliepa zengwe zima.

Mawaziri waliotia fora kummaliza jamaa ni wale walioghushi vyeti vya taaluma na wale walioendekeza ziara nje ya kaya. Hata katibu wa CCM mgosi Makambale naye amemuangusha sana bosi wake kwa kuwa kihiyo na mwongo tena mwenye kuwakejeli walevi na kujipendekeza kwa bosi ili aendelee kula.

Pia marafiki na washirika zake ambao hakukutana nao barabarani yaani Eddy Ewassa, Bazie Rambarambapesambili, Endelea Chenga, Roasttamu Kagodoka na wengine, walimwangusha chari.

Kwani walimkaba shati kuwa lazima awapigie kampeni na asivyofanya hivyo wangemwaga mtama kwenye kuku wengi. Hivyo walevi wameamua kumnyima kura ili kuona kama mafisadi wenzake hawa wataweza kumpa kura za kula za kutosha.

Pia bi mkubwa na kitegemezi chake nao wamewatisha wapiga kura. Kwani wamekuwa wakitoa matamko kama marais ukiachia mbali kutumia fedha na raslimali za umma kujenga biashara ya ukoo yaani kuusaka ulaji kwa mgongo wa kodi za walevi maskini.

Kundi jingine ni lile la vyangudoa wa kimaadili yaani wahandisi wa uongo waitwao waandishi wa habari. Kundi hili ambalo linamramba jamaa visigido limewatia kinyaa walevi kwa kuwachafua wagombea wengine na kummwagia sifa za uongo jamaa wakati likijua hana bao wala sera. Hata sura yenyewe siku hizi imeanza kuvia kutokana na uzee, mieleka, maradhi na mambo mengine ambayo ni siri.

Gesi la Watawala yaani DWTZ limemmaliza mkuu kwa kutoa vitisho kwa wapiga kura na walevi.

Mapendekezo ya Kedet

Mosi, Mkuu kutogombea. Kama angeacha mwanachama mwingine mwenye udhu na akili agombee huenda matokeo yangekuwa tofauti. Lakini hili hakulifanyia kazi.

Pili, alipaswa kutaja mali zake, mkewe na mwanae hasa tuhuma kuwa anamiliki bungalow la madafu bilioni. Pia alipaswa kuwafikisha kwa Pilato mifasadi na washirika zake wote ili wafungwe na kunyang’anywa mimali waliyokwanyua.

Tatu, chama cha maulaji kivunjwe au kurejeshwa kwa makapuku waliokianzisha wakati wa nabii Musa.

Nne elimu ya uraia itolewe hadi kwenye mabaa na madanguro huku maandamano yakiingizwa kwenye katiba.

Tano, njuluku zilizopatikana kutokana na ufisadi, mikataba, uuzaji wa magogo, uuaji wa wanyama vitalu na migodi zilizotoroshwa zirejeshwe nchini. Hapa kampuni la Deep Green wa magrini lilitia fora kwa kutoroshea njuluku nje ya nchi hasa kwenye visiwa fulani.

Sita, wanakaya wasipewe aiskrimu takrima kwenye uchaguzi wala ahadi hewa na za hovyo.

Saba kiongozi atayeunguza kwa kuongopa atiwe bakora hamsa na kushushwa jukwaani huku akizuiliwa kushiriki siasa maisha.

Saba, wabunge wazururaji wasingeruhusiwa kugombea.

Nane, ameshindwa kupata suluhu ya migogoro ya miungano kama ule wa Zenj. Muungano uvunjwe kuepuka migogoro na mitafaruko huku kiranja wa Zenj akichaguliwa na wanakijiwe wa Zenj kwa maelekezo toka Zenj siyo Idodomya.

Kitu kingine kilichobainika kwenye utafiti ni kuchoka kwa katiba ya Kaya ambayo licha ya kuwa na viraka ni ya mwaka 47. Kedet inapendekeza iandikwe mpya kwa kasi mpya, ari mpya, nguvu mpya na watu wapya.

Tisa, Kedet inapendekeza kosa la ukeketaji wa kimawazo liingizwe kwenye Penal code au kanuni ya jinai na adhabu ndogo ya miaka 50 itolewe kwa watakaotenda kosa hili.

Kedet ina mpango wa kuchapisha kitabu chenye kurasa 1000 kuelezea upya jinsi Kaya inavyoweza kurudishwa kwenye hadhi yake aliyoiacha Musa kabla ya Farao na Delila kuinajisi Kaya takatifu ya watulivu na wenye mapendo vitu vinavyoanza kutumiwa na mafisadi kuwaumiza wanakaya.

Taarifa hii imeandaliwa na Profesa emiritus Mpayukaji Msemambovu wa Kedet. P.o Box Mafichoni kwa Mfuga mbwa.
Chanzo: Tanzania Daima Oktoba 13, 2010.

No comments: