The Chant of Savant

Thursday 28 October 2010

Nimekuja na gea mpya kutaka kura

Baada ya kuona maji yanazidi unga huku kitumbua changu kikianza kuyoyoma, kwa vile nimetangaza dhahiri nitaingia Ikuu, nimekuja na mikakati mipya ya kukata na shoka.

Tumeweka mikakati mingi kuhakikisha tunashinda japo mambo yanakwenda ndiyo siyo kwa sasa. Tumegawana kaya mimi bi nkubwa na kitegemezi chetu na mashoga zao. Mkakati mwingine ni kuhakikisha tunachakachua ima kwa kuchukua na kuweka waa au. Kuhakikisha hili tumeishaandaa mazingira ambapo tunatumia utafiti wa kishikaji unaonifagilia ukiwaponda wenzangu ili hapo tutakapochakachua tuutumie huu utafiti wa washikaji wetu ambao tunawalipa kuhalalisha uchakachuaji wetu.Ukiwa na njuluku na wasomi wa nepi ambao wako tayari kufanya kila upuuzi wako hukwami sana.

Hii ikishindikana, tutaingia kwa fosi yaani kuwatumia vijana wa dolari kutembeza kipigo kwa wasimamiaji kula watakaokataa mshiko ili tufanye vitu vyetu. Tuna uzoefu hasa tukitumia ule uzoefu wa kule Zaainzibaa miaka iliyopita. Tulishalianzisha kwa kuwatumia washikaji zetu kwenye fosi ambao mambo yao si haba huenda kishimbo shimbo. Ingawa wengi wamestukia mkakati huu, watake wasitake hatuwezi kuondoka kwa vipande vya karatasi hata kidogo.

Mkakati mwingine ni kujifanya mnyonge na mwenye kuwajali na kuwapenda na kuwahusudu wanyonge hasa wazee na walemavu ambao nawatembezea takrima ya bajaj na magari ili kuwazuga wengine. Hamkuniona nikaa kwenye matope huku wapiga picha wangu wakinipiga picha kama hawana akili nzuri? We ngoja niukwae tuone kama mtaniona nikidhalilika hivi. Kula si mchezo lazima uwe bingwa wa sanaa hasa za maonyesho. Nani aliwahi kumnasa samaki bila kuweka chochote kwenye chambo?

Hamkuniona nikijichanganya na hata kuwapa shikamoo watoto na kutoa rushwa sorry zawadi mbali mbali ukiachia mbali kupandisha hata mshiko wa baadhi ya watumishi wa kaya? Msidhani mie njinga. Nafanya hivi ili muingie mkenge halafu tuwakomeshe. Na ikitoka hairudi. Maana sina mpango wa kugombea tena zaidi ya kuweka kibaraka wangu ili hapo baadaye alinde maovu yangu.

Kuhakikisha walevi hawastuki, nimewaagiza baadhi ya vibaraka wangu kuhakikisha wanapiga magoti kwenye michanga wakati wakiniombea kura bila kujali wana PhD za kweli au kughushi. Nataka waonekane watiifu hata kama ni wahalifu.

Mkakati mwingine ni kuhonga bajaj ili nikipata ulaji ninunue mishangingi. Kuna ndude imegunduliwa nchini Ukanada inaitwa Knight XV. Nasikia inauzwa dolari 800,000. Nikishinda lazima ninunue hizi kwa ajili yangu, mawaziri, bi mkubwa, kitegemezi na mashoga zao ili tufaidi sawa na walevi watakavyokuwa wakifaidi bajaj zetu.

Kweli walevi ndio waliwao. Unawahonga bajaj wanakupa ulaji wa kufa mtu? Unakula wewe, bi nkubwa na mashoga zake, vitegemezi na maswahiba wengine. Mwe! Najisikia kupasuka kwa furaha. Acha wanipe raha. Nikishapata raha nawapaka kuwa raha wajipe wenyewe wasingoje kupewa na wasanii kama mimi.

Mkakati mwingine ni kutumia vitisho kwa kupitia mtabiri wangu na masoja walio washikaji wangu ambao nilishawapa ulaji wakahomola kama yule Shimboka.

Mkakati mwingine ambao ndiyo mtaji wangu mkubwa ni kuwachafua wenzangu kwa kutumia waandishi vyangu. Hamkusikia wakimkandia jamaa kuwa alikwipa kidosho cha mtu wakati mie ninavyo milioni? Mkakati huu kiasi fulani haukufua dafu. Hata yule shangingi wa kinshomile Silvia Rweyependekeza aliyeubuni miaka iliyopita anaonekana kuishiwa mbinu kutokana na kumpa ulaji akageuka bomu. Akiendelea na ujuha wake mie nitamtimua nimweke shangingi jingine la kinshomile liitwalo Mihingulo Rweyependekeza. Maana naye naona anajipendekeza kiasi cha kunikuna.

Mkakati mwingine ni kutumia majuju majini na vitisho vya kishimboshimbo ili walevi wajue wasiponichagua nitavuruga amani ya kaya kwa kuwatumia watu wangu ambao wako tayari hata kuniramba manonihino nikisema. Mie ni chaguo la God, Majini masoja na hata wadudu. Mpo hapo vichaa wangu?

Inabidi walevi wajue fika kuwa amani ya kaya ni kuniacha mimi na watu wangu kula kaya kama hatuna akili nzuri. Asiyekubaliana na hili anatishia amani ya kaya ambayo kimsingi inategemea na kuniacha mie na watu wangu tukitesa kama hatuna akili nzuri hata kama ni kwa walevi kuteseka.

Wanaohoji tunavyopunyua njuluku za kaya na kuwekeza kwenye kampeni za ulaji wetu hawaitakii kaya amani.

Mkakati mwingine ni kumwaga ahadi kama sina akili nzuri. Walevi wengi, kwa kupenda vya dezo na kukosa kumbukumbu watanipa ulaji wasijue wataliwa wao. Mpaka sasa wataalamu wangu wameniambia kuwa nimeishatoa ahadi zenye thamani ya pesa ya madafu kitu kama Zillion mbili! Manijua Zillion wasomaji? Ni kiwango kikubwa cha pesa ambacho hakijawahi kuwapo duniani tangu kuumbwa kwake.

Bila kuwafunga walevi kamba hupati kula. Kwa vile walevi wanapenda sana kuahidiwa uongo na uongo haunigharimu kitu, lazima niongope kama sina akili nzuri. Kipindi hiki nitaahidi kuwapeleka walevi kumuona Mungu wakiwa hai. Mambo ya Kanani yamepitwa na wakati. Mambo yote ni kuwapeleka walevi kukutana na Bwana God ambapo watapewa ulabu kama hawana akili nzuri. Asiyeamini ukweli huu anatishia amani ya kaya na vijana wangu wa Red Brigade watamtia adabu kwa kumwaga damu yake.

Mkakati mwingine tuliobuni ni kukacha midahalo ili tusiadhirike kutokana na viherehere wengi kutaka tuende kule watuvue nguo. Sisi tunategemea ujinga wa walevi. Hivyo ijulikane kuwa walevi huwa hawana muda wa kutazama luninga. Kwanza hawana luninga na wakiwa nazo hawana umeme na wakiwa na umeme wanaangalia michezo ya kuigiza ya Nigeria na mpira wa mateke wa Uingerezani. Hata magazeti yenu ya udaku wa kisiasa hawasomi. Badala yake wanasoma yale ya udaku wa ngono na upuuzi mwingine. Unacheza na wapuuzi sorry walevi nini? Hakuna mtaji mzuri kwetu kama ujuha na ujinga. Na bila kuondoa hili wanaotaka siti yetu walie kwa sana tu.

Pamoja na mie kuwa kilaza, hata ningekuwa na ubavu nisingekubali kujitia kitanzi kushiriki upuuzi huu wa kuvuana nguo. Mlitaka niende nikaulizwe nilitekeleza nini na kushindwa nini siyo? Nimewastukia. Kaya hasa ya walevi ahitaji kuwa na mkuu mjuaji zaidi ya msanii. Ebo! Mshikwe wapi mstuke? Muambiwe nini muelewe kuwa mtaliwa ad infinitum this time around. This is cinch to happen. Kumbe ulabu umepanda hadi namwaga umombo!

Tena ngoja niwahi mechi ya Manchester nikamuage Rooney Wayne.
Chanzo: Tanzania Daima Oktoba 27, 2010.

No comments: