The Chant of Savant

Thursday 9 December 2010

Siku ulipokatiliwa ushauri wa kuokoa pesa ya walevi

Mwenzenu juzi nilikuwa nimejichimbia Bwagamoyo. Msianze kupayuka kuwa mzee mzima nimeamua kufuata dini za kishirikina za jamaa zangu. Hizo nimewaachia waganga njaa kama Shehe Njaa Yahya na wanaojiita viongozi wa kondoo wakati ni mbwa mwitu na mafisi ya kawaida yaliyojificha kwenye ngozi ya kondoo.

Niliitwana Mkuu mwenyewe na rafiki yangu mkubwa ingawa mie si mshiriki wake, Njaa Kaya ili kumpa tafu kwenye kuunda kabineti ya ulaji.

Kabla ya kwenda, ilitangazwa bombani kuwa ameniteua kumshauri katika kuendeleza libeneke hili. Baada ya wapenda ulaji kusikia vile, walinisumbua sina mfano. Mara wanipigie simu. Mara waniandikie emails, barua pepe na meme. Walimemetuka kwa kimuhemuhe na kujaa mapepe. Mie niliwaambiwa openly kwamba waende kwa mwanae na mkewe kwani mi si wa hovyo hivyo. Mie si mtu wa kumlamba mtu matako bwana eti anitupie makombo.

Wengi walijikomba hadi wakatapeliwa na wasaka ngawira waliomzunguka bwana mkubwa. Yote juu ya nini? Kupata mwanya wa kuchakachua mipesa ya wanuka jasho wa Danganyika.

Baada ya kufika kule Bwagamoyo, sikuamini macho yangu. Nilikuta umati mkubwa wa wataka ulaji ukijidhalilisha kwa jamaa yangu utadhani mfalme wa nchi ya kiarabu! Watu wazima waligeuka kama vyangu katika kujikomba na kujirahisi ili wapate ulaji wa dezo.

Nikiwa natafakari hili na lile, mara nikakaribishwa ndani tayari kuanza zoezi la kuteua walaji wenu. Baada ya kuamkuana na jamaa huku akinitupia lawama lukuki kwa kumnyima tafu, nilitoa masharti ya kufanya kibarua kile.

Sharti la kwanza ilikuwa ni kuhakikisha wale wote waliotuhumiwa kughushi nyaraka na vyeti vya shahada na digrii anawapiga chini. Mwe! Jamaa alibadilika. Yule Chekacheka tuliyemzoea alitoweka ghafla na kuingia Nunanuna. Bila hili wala lile alianza kunishushia shutuma badala ya wale walioghushi.

Sharti la pili ilikuwa ni kuhakikisha hakuna cha shemeji wala mtoto wa fulani. Hili nalo nusu limpasue jamaa. Hii ikichanganyikana na afya yake yenye ugogoro ndiyo usiseme. Kabla sijatulia hata kunywa mvinyo uliokuwa ukiningoja mezani, jamaa aliamka na kunionyesha mlango.

Nilipokuwa nikitoka akaniita. Kwa vile mie huwa sina dogo na sitetemekei miungu watu, niliamua kujitoa kama sina akili nzuri. Nilipikigiza mlango na kuishia.

Kwa vile jamaa anajua hasira na busara zangu, hakuwambia uhasama wa taifa kunizuia. Maana ningewatia adabu na kuwaletea aibu hakuna mchezo. Ananijua kuwa mie ni gwiji la jet kune doo na wu shuu ambazo zote nina mikanda ya dhahabu na shahada ya juu ya upigaji karate na judo.

Hivyo hakujisumbua na kunizuia hasa ikizingatiwa mwenembago wangu akipanda naweza kumwadhibu yeyote bila kujali ukubwa wala nini.

Nilitoka nje na kumwamrisha dereva wangu anirejeshe kwangu nyumbani.

Nilipofika nyumbani, kinokia changu kikaanza kuhanikiza. Kucheki namba kumbe Njaa Kaya mwenyewe.

Alijitahidi kuniomba msamaha kwa yaliyotokea huku akiahidi kunitumia helkopta nirudi Bwagamoyo au yeye aje kwangu nimsaidie kibarua kile. Nilimwambia wazi wazi kuwa kama hatatimiza masharti yangu mie sitakuwa tayari kujichafua kama yeye kwa kulala kitanda kimoja na wahalifu.

Tukiwa tunaongea, alitaka kujua ni kwanini nilikuwa na masharti na msimamo mkali. Nami bila kujali ukubwa wake wa kupewa kwa vile namwogopa Subhanna pekee, nilipa sababu za kuja na masharti makubwa vile. Nilimkataza kuendeleza ushikaji na kubebana kwa kuangamiza umma hata kama haufurukuti. Nilimuonya kuwa kuna siku umma utaamka na kufanya kitu ambacho kitawashangaza wengi.

Kumkatisha tamaa, nilimkaripia na kutoa sharti jingine ambalo ilikuwa ni kwamba siku akiutangazi umma wa walevi uteuzi wake, nilitaka atangaze sambamba na hili, kuwaweka ndani watuhumiwa wote wa kughushi na wale wa HEPA na Richmonduli.

Hili lilimchanganya hadi nikasikia sauti yake ikianza kukoroma. Ghafla nilitegemea ningesikia aisee mara ntiii. Lakini haikutokea na kama ilitokea basi wambea hawakuipata.

Niliendelea kumpa sababu ni kwanini nilikuwa na masharti ambayo kwangu yalikuwa ni rahisi ingawa yeye aliona magumu.

Kwanza, lengo langu ilikuwa ni kuhakikisha wale wote walioghushi kama kina Emmy Nchimvi, Bill Waling'ombe Lukuvile, Merry Nyago, Makorongo Muhanga na wengine hawarejei. Ingekuwa laana na aibu ya namna yake kama ningeshiriki kwenye kurejesha wahalifu ulajini ilhali wanapaswa kunyea debe kule lupango.

Hakuna kitu kilinitisha kama kusoma CV ya Emmy Manu Nchimvi. Eti anasema alisomea PhD na masters kwa pamoja tena toka kwenye chuo kinachotia kila aina ya shaka. Haijawahi kutokea. Hata Newton, Galileo, Ensteins nami hatukusoma digrii zetu kwa muda mfupi hivi tena kwa pamoja. Kama sisi na ugwiji wetu tulishindwa inakuwaje kilaza mmoja aweze? Hilo utajibu mwenyewe.

Nilipoangalia CV ya Bill ndiyo nilikaribia kupata kichaa. Ukiondoa cheti ya upiga chaki yaliyobaki ni uchakachuaji mtupu. Hivyo kwa ufupi nilikataa kushiriki jinai hii.

Pili nilitaka watu kama Husseinu Muinyi aliyezembea hadi mibomu ikaua watu kule Mbagala nilitaka atemwe bila kujali kuwa ni mtoto wa aliyemtengeza jamaa yangu. Pia nilimweleza kuwa watu kama Hawa wana Ghasia sikumtaka tena kwenye ulaji kwa vile hakuwa na sifa zaidi ya ushemeji wala mkwe wake mzee wa Ruxa. Pia nilimtaja mtu kama Porofwesa J4 Majembe. Huyu alivuruga elimu. Kuna watu kama Joji Mkunjika na Shukuruni Kawa-Mbwa. Hawa waliboa sana kwenye ngwe ya awali.

Kwa vile jamaa ni mugumu wa kuelewa na kujifunza, baada ya kuona anaendelea kutetea uoza nilkata simu na kumuonya asizidi kunipotezea muda. Nilimshauri kuwa kama angetaka ushauri basi angewaalika Bi Mkubwa wake mpenda sifa na rais wa MAWAWA na kitegemezi chake Riziki One Tegemezi.

Kabla sijasahau, siku moja kabla ya kuitwa Bwagamoyo, nilikuwa nimempigia simu Jamaa kumuonya juu ya uteuzi wa Jan Makambale. Nilimuonya baada ya kusikia mgosi Machungi Makambale akijisifu kuwa lazima kitegemezi chake kiule.

Sambamba na la mtoto wa Makambale nilimuonya kuhusu kumrejesha Ewassa kutokana na fununu nilizo kuwa nimezinyaka. Ingawa alijifanya kutumia timu ya familia yake, naona alitumia baadhi ya ushauri wangu.

Pia nilikuwa nimemshauri aunde kijibaraza kidogo tu na siyo genge kuubwa tuliyojaziwa walaji. Kwa vile jamaa yangu ana domo kubwa na hana masikio, ameendelea kuwaumia walevi bure. Hata hivyo hapa wa kulaumiwa ni walevi wanaoendelea kumuendekeza badala ya kumtolea uvivu maana njuluku wanazokwapua hawa jamaa zake si zake bali walevi.

Don't take me seriously. You know what?

I am just dreaming.
Chanzo: Tanzania Daima Desemba 7, 2010.

No comments: