The Chant of Savant

Friday 14 January 2011

Tunisia wamtimua rais fisadi na imla

Ben Ali pichani






Kwa wapenda mageuzi na demokrasia barani Afrika na Dunia kwa ujumla, kilichotokea Tunisia usiku wa kuamkia leo ni ushindi na zawadi ya mwaka mpya. Imla wa nchi ile aliyeitawala kwa zaidi ya miaka 20, Zine al-Abidine Ben Ali alilazimika kuyatema madaraka baada ya waandamanaji kudhoofisha utawala wake nchi nzima.

Baada ya kugundua kuwa maji yamezidi unga na hawezi kushindana na nguvu ya umma, Ben Ali aliamua kutimua mbio akikasimu madaraka ya rais kwa waziri wake mkuu Mohamed Ghanouchi ambaye amejitangaza kuwa rais wa mpito.
Ghanouchi ametangaza kuwa atakaa madarakani kwa muda huku akishauriana na wadau wote nchini juu ya mpito mzima.

Kosa kubwa alilofanya licha ya ufisadi ni kuamuru polisi kuua waandamanaji waliokuwa wakipinga ufisadi wake. Watu wapatao 23 wanasadikiwa kuuawa na polisi hadi imla huyu akikimbia kuelekea ima Ufaransa ambapo inasemekana amekatazwa kutua au Montreal ambako mkwe wake ana nyumba.

Ukiangalia kilichotokea Tunisia hakina tofauti na kilichopaswa kutokea Tanzania baada ya mauaji ya waandamanaji waliokuwa wakipinga ufisadi. Hili ni somo muhimu kwa watanzania kuwa umma ukishikilia madai yake wezi wanaweza kutimka na familia zao kwenda kuishi ukimbizini bila manjonjo na makandokando ya madaraka.

Rais Barack Obama wa Marekani amewapongeza waandamanaji kwa kuwa na mioyo mikubwa hadi kumtimua huyu mwizi mkubwa. Kwanini watanzania wasiingie tena mitaani kuhakikisha Bwana Dowans son of Kagoda the grandson of EPA anatimka na wezi wenzake?

Maswali muhimu ni je kwanini Tunisia waweze Ivory Coast washindwe? Je wezi na maimla wa kiafrika wamejifunza nini? Je huu ni mwanzo wa mapinduzi matakatifu ya kuondoa watawala wezi, wababaishaji na mafisadi?

Laiti Uganda, Rwanda, Sudan, Tanzania, Zimbabwe, Congo-Brazzaville, DRC, Equatorial Guinea,Ethiopia na kwingineko kwenye watawala madikteta na wezi wangelishika somo hili.

No comments: