The Chant of Savant

Wednesday 27 April 2011

Majoka yanapovuana magamba

KITENDAWILI? Tega. Ni chata gani linasifika kwa kuwa chata la majoka? CC. We koma. Hata kama ni Chama cha Majoka (CCM si ile ya Chama Cha Mapinduzi) tuwaache na unyoka wao.

Waweza kuamini kuwa juzi nilikuwa maeneo ya Dom kutaka kushuhudia majoka yanavyovuana magamba? Basi mwenzenu niliingia kinamna tena bila kujulikana. Hata mnoko Makambale wakati anafurushwa akilia lia na kukamia wengine nilishuhudia.

Hata Ewassa, Rostatamu, Endelea Chenge walipokuwa wakipanic niliona. Hata Chekacheka alipowatuma waramba viatu na viherehere wake kina Makarongo walibumburuwe niliona.

Hata wale walevi wa ofisi za chama walipokuwa wakishangilia Makambale kupigwa chini niliona. Kimsingi niliona kila kitu isipokuwa sikuona gamba hata moja likivuliwa.

Waweza kuamini? Niliingia kwenye gwena hili kwa siri kubwa sana. Maana, kama ingejulikana kuwa nilikuwamo kwenye kigwena chao ningezongwa na mashabiki wangu kiasi cha wengine kuona wivu na kuita wale mafyatu wa Fanya Fyoko Ukome (FFU).

Hata hivyo good news ni kwamba wameula wa chuya. Maana sasa tutashuhudia maswahiba wakitaka kutoana roho kwa kutumia njuluku hizo hizo za ufisadi. Hapa taka usitake, amini usiamini ni mbwa kala mbwa.

Maana kilichoitwa kuvua gamba si kuvua gamba bali kugeukana. Wahenga walisema: jinai hailipi. Hata hivyo ni furaha yetu kuona majambawazi yakigeuziana mitutu. Vita ya kunguru bwana! Halo halo! Una dola wewe? Una udhu wewe?

Je, watafanikiwa kuwahadaa walevi kama ambavyo wamekuwa wakifanya kwa kukanusha ukweli ambao hata kuku wanaujua? The gut-wrenching reality is the fact that you can be darn sure. If walevi don't watch these winos and their mealy-mouthed lies, they will be screwed up come high rain come shine.

Samahani, nimepandisha Mwenembago hadi ung’eng’e wa uhakika unanitoka bila kudhamiria. Niseme tena kwa herufu kubwa. Hakuna cha kujivua gamba bali kuwazuga eleweni mtaliwa mwajiona shauri yenu.

Watu wenye akili wanauliza: je nyoka akijivua gamba anaacha kuwa nyoka? Unyoke wa nyoka si magamba yake bali sumu yake. Hivyo, niseme wazi. Nyoka bado ana magamba tena mengi tu. Kama wanataka kumshughulikia nyoka vilivyo kwanini wasimpondeponde kichwa au hata kukikata?

Kama wameshindwa kwa kuoneana huruma si waniambie mzee mzima niwashikishe adabu nyoka wao? Kama hawaniamini mimi basi wawapeleka hao majoka kwa Pilato hata lupango. Wakifanya hivyo tutawaelewa. Hata hivyo kuna swali gumu kuu. Ni nyoka yupi amvue gamba mwenzake wakati wote ni majoka?

Mnaletewa shehe wale wale kanzu tofauti. Wana nini hawa vimbelembele walioletwa? Hebu watazame. Huyu Mape Naye naye ana nini jipya zaidi ya kuimba wimbo ule wa jogoo?

Je, yeye si gamba la gamba sawa na warithi wenzake wa nafasi za baba zao? Asingekuwa mtoto wa joka nani angempa ulaji? Juzi nilimsikia kwa masikio yangu akisema eti wasimsakame joka kuu kwa vile yeye hana magamba! Ebo! Huyu nyoka mchanga hajui tunajua alivyo tunda na matokeo ya nyoka?

Kinachofurahisha ni kwamba akina Mape wa Mapepe wanajihadaa kama walivyofanya akina Kibaraak na Gbadboy. Siku yao ikifika watajikuta pakanga wasiamini. Hata wenzao walijihadaa hivi hivi wasijue mambo yamebadilika na walevi wamefyatuka.

We ngoja hii njaa iliyopiga hodi na maisha kuwa machungu vizidi kukaza uzi. Lazima walevi watachenji na kufanya kweli.Maana wahenga walisema: adui yako muombee njaa. Tuombe njaa na ughali wa maisha viumke tuone kama wataendelea kutukejeli kwa kujifanya wanavuana magamba wakati ni usanii.

Kabla sijasahau, nadhani mliipata ya dokta Silaha ya juzi kuwa kumbe kile kinyoka kichanga kiitwacho Ziliwani ni bonge ya bilionea! Nakumbuka. Tulikuwa wote pale Ikungi kwa wanyampaa. Nani akanushe tumvue nguo. Kwa taarifa yenu tuna data zote za mafisi na majoka. Tunangoja waanze kuchenjiana tuwaweke pakanga bila huruma.

Juzi nilifurahi sana pale Idodomya. Maana yule Jambazi wa visenti, Ewassa na Roasttamu walinywea kama mijibwa iliyoloa chapa chapa. Sikusikia tambo na jeuri za awali. Nyeti nilizopata toka radio mbao ni kwamba Roasttamu ameishauza kila kitu chake na anataka kurejea kwao Uajemini. Je, hawa majoka wetu watakimbilia kwao wapi wakati hawana kwao kwingine?

Tuulize tena kwa upole ili watuelewe. Je kurithishana maulaji siyo gamba? Yupo huyu Andraman Kinamna. Mbona zali lake la nyara haliongelewi? Au wanadhani tumesahau? Kwanini naye asivuliwe? Kwanini ufisadi wa kina Ewassa uwe dili lakini wa akina Kinamna hata Njaa Kaya na sasa kitegemezi chake Riz-One uwe Baraka?

Je, watafanikiwa kuwavua wengine gamba wakati wao wakibaki na magamba yao? Huwa sina uhusiano mzuri na Ewassa na wenzake. Simtetei. Ila nataka haki itendeke na si kuhadaana na kutoana kafara. Kwenye Richmonduli alitolewa kafara. Na sasa mnamtuoa kafara tena! No it can’t be. Ewassa, mwaga tama kuku tutafune ili nao waaibike. Maana huna cha kupoteza. Kama ni kuchafuka ulishachafuka na kunuka sana mshirika.

Usiogope. Mimi ni lawyer wa malawyer nitakutetea kwa pesa kiduchu. Ila sharti njuluku hizi zisiwe zile ulizokwapua. Mie si fisi wala fisadi. Sitetemekei upuuzi uitwao pesa ya mafisadi.

Muhimu uelewe utetezi wako ni rahisi. Maana, List of Shame ambayo ni shame of the nation bado haijabadilishwa zaidi ya kuzidi kupata washikaji wengine hasa wale waasisi wa HEPA iliyogharimia mbio za Njaa kuupata ulaji.

Kabla ya kutimua niseme kitu kimoja. Dk. Silaha ameniudhi kwa kutomtaja Pita Nonihino no ni… Ambaye naye alishirikiana na akina Dugong Benny kukwapua njuluku za HEPA.

Naona kile ki-Makambale Juniya nacho kinazidi kupanda kuchukua nafasi ya kayaya mwenyewe. Hapa kuna jipya au kuhadaana. Ukimtazama yuke Zaakia Mengijii unashangaa mantiki ya mikelele yote ya nyoka kujivua gamba. Huyu nani kasahau aliidhinisha EPA ukiachia mbali kuchafua hewa kwenye wizara ya mahayawani mwitu? Juzi nilimdeku akiwa kwa Joji Kichaka na shoga yake rais mama wa MAWAWA na mwanasheria wa HEPA, Mwana wa Idi Maajaraa wakitanua na kufanya ufisadi kwa kutumia cheo cha jamaa.

Tumeshawashtukia hata mkila jiwe. Nanyi mwapaswa kuvuliwa magamba hayo. Hivi mshirika wangu Anna Tamaa Makapi ameishia wapi? Kweli avumaye baharini papa wengine michosho. Leo upo juu kesho down tunakucheka. Hata mvuane nguo mtabakia kuwa mafisadi.

Naona kina Mape na Makambale juniya wale. Ngoja niwasogelee na kuwaramba vibao majoka hawa. Rais mtarajiwa.
Chanzo: Tanzania Daima Aprili 27,2011.

No comments: