The Chant of Savant

Friday 27 May 2011

Kumbe bei ya mlevi mmoja ni vipande vitatu!

MWENZENU nina mipango bab kubwa ya kuwakomboa walevi na wadanganyika kwa mpigo. Ingawa Geronimo EKIA, mie napanga kuwa mkaidi. Sitalala kitanda kimoja na mafisadi wala kujigeuza changu kwa bei yoyote.

Sitatishwa wala kuhongwa hata kwa mabilioni ili niwauze walevi wangu. Mie ni maskini jeuri na si changu kama wale wanaofakamia uchafu wa mafisadi wa nje huku nao wakigeuka mafisadi wa ndani hata wawe na power.

Tofauti na wale magaidi uchwara wanaotumia dini, mimi nasema wazi kuwa nataka kuanzisha kundi liitwalo al-Kaidi. Nimechagua jina hili kuonyesha ukaidi wangu na si ugaidi.

Mimi kama kiongozi wa mtandao wa al-Kaidi sitajificha kwenye mahekalu huku nikiwahimiza walevi wajitoe mhanga wakati mie natanua na washirika wa bedroom kama Osami bin Burden aliyepunyuliwa hivi karibuni. Huu kwangu ni woga na unafiki. Lazima jemadari aongeze mapambano badala ya kuwatuma wengine wateketee yeye akitanua. Jemadari wa namna hii kwangu ni mwoga na changu wa kawaida.

Mie nitatumia watu wenye uchungu na kaya yao badala ya majuha waliochoka kuishi wakitafuta pepo kwa kuua wenzao. Mungu si mpuuzi kiasi hicho kuruhusu uue ndiyo uingie peponi. Pia Mungu si mchovu kiasi cha kutegemea ngurumbili wasio na maana kama hawa ninaosema. Mungu wa kweli ahitaji msaada wa binadamu kufanya mambo yake.

Mungu wa namna hii ni mchovu na kuogopwa kama ukoma. Leo sitaongelea sifa za Mungu. Kwa hicho kiduchu ngoja niachie hapo na kuelekea mambo mengine urgent.

Hakika, matandao wangu hauna dini kama ipo si nyingine zaidi ya uzalendo. Pia, sitawaahidi wafuasi wangu kwenda peponi zaidi ya kutengeneza pepo hapa hapa kayani. Napanga kufanya mambo yanayoingia akilini badala ya wendawazimu kama wale wachovu wa madevu aliyepunyuliwa hivi karibuni.

Lengo la kundi langu ni kudai haki ya wabongolalalanders wa Danganyika kwa kukaidi upuuzi wote kuanzia propaganda, hongo, vitisho na ujambazi mwingine. Hivyo, hata kama nikiitwa gaidi roho haitaniuma kwa vile ninachopanga kufanya si uganga njaa wa kumtumia sir God.

Mie nasema wazi. Nitapambana na mafisi na mafisadi wakiongozwa na Njaa Kaya na ukoo wake na walamba viatu wake wakiongozwa na Rostitamu na shangingi la kinshomile Silvia Rwependekezamu.

Hakuna kitu kimenichochea kuanzisha al-Kaidi kama mauaji ya kinyama waliyofanyiwa walevi wa kule kwa kina Mura Msama wa mbuye ori tata? Nimeamua kufanya hivi kutokana na kuona kuwa jamaa hawa wanaosifika kwa kujiamini na kulipiza kisasi kushindwa kuwanasa angalau vibao wale wakubwa wa genge la mauaji walioongozwa na Po Chagonjwa kwenda kuwahadaa eti wakubaliane na upuuzi wa lisirikali wazike wafu wao.

Hata hivyo nawapongeza kwa kunusuru kumnyotoa roho msaliti wao mkuu Nyambwari Nyangwile. Kitendo hiki kitaandikwa kwenye historia ya ukombozi wa kaya kwa maandishi ya dhahabu na vito vya thamani. Tusibweteke na hili. Tuwafanyie kweli ili tujikomboe kweli.Nasema tusibweteke kutokana na ujinga tunaofanyiwa. Watu wanauawa halafu wahalifu na wauaji waliofanya hivyo wanasema waliodedishwa ni wahalifu! Hivi kuna tusi baya kuliko hili wandugu zanguni?

Yaani tumekuwa wa hovyo kiasi cha kuvumilia matusi kwa marehemu zetu waliorudisha namba wakipigania heshima na haki ya kaya yetu! Je hawa maiti si bora kuliko sisi?

Twazidiwa na hayawani mdogo kuku ambaye yuko tayari kufa akipambana kuokoa vifaranga wake kuliko kuendelea kunenepeshwa kwa mahindi ya amfugaye! Hata kondoo hufikia mahali wakakereka na kutembeza kichapo. Duh! Hata hayawani wanatuzidi. Je, sisi ni hayawani kuliko hayawani?

Mandata wakae mkao wa kula. Maana zali langu lazima lianzie kwao ili waache kujigeuza mbwa wa kutumia na genge la mafisadi wenye power.

Tujikumbushe. Ji jitu limoja liitwalo Kangacheki lilikaririwa na vyombo vya umbea likisema kuwa watu waliouawa kule ni majambawazi. Mie nasema walionyotolewa roho ni mashujaa. Anayesema ni wahalifu ni mhalifu na kumbaff.

Hebu tutumie common sense japo kwa chati. Sasa kama kweli hawa watu walikuwa majambazi mbona lisirikali lilitoa madau milioni tatu kwa kichwa ili maiti wafukiwe na ushahidi wao?

Ingawa msiba huu umeniumiza na kuniathiri kisaikolojia, umenifumba macho kuwa kumbe bei ya walevi ni ndogo kuliko hata babaj!

Ya kwa akina Mura Msama tisa. Wajua kuwa kaya sasa inauzwa kwa maponjoro na magabacholi? Kama hujui jua sasa. Bado wake zenu na mama zenu. Bahati nzuri bi mkubwa wangu alishakufa.

Nimeamua kuanzisha kundi langu la al-Bamiza kuhakikisha mshirika wangu wa bedroom na dota wetu hawapigwi mnada na hawa mahabithi. Hivi wakija nanyi mtauzwa?

Je, wajua? Hawa mahabithi wanafanya kufuru zote hizi kwa imani kuwa walevi na makondoo na njiwa. Mie simo. Maana wanatuuza sisi na ardhi yetu ili wao na wabwana zao waendelee kutanua siyo?

Loh! Nilitaka kusahau. Umesikia tangazo hili? Mheshimiwa alhaji Mpayukaji anafurahi..sorry anasikitika kutangaza kifo cha shehe Yaya Hoseni kilichotokea Mwembamaziwa na habari ziwafikie washirikina wote wakubwa na wadogo.

Misiba wa sheheha shehe Yaya Hoseni nilioutabiri. Nawashauri wenye mamlaka waliokuwa wakimtumia waje kwangu mara moja maana mie natabiri ukweli. Mkuu upo? Chama cha manonihiino mpo?

Je, vais tue quelque granuile qui voleur nos argents. Je crois que je vais success vraiment. Usishangae na kuuliza hii lugha gani. Hiki ni kifaransa na tafsiri yake ni simpo:nitaua chura yoyote anayeiba pesa yetu niamini.

Nimalizie kwa kitendawili. Je bei ya mlevi ni gani? Just madafu milioni tatu.

Naona wale ndata wanafanana na wale waliodedisha watu wangu kule Tulime. Acha nikawazabe vibao. Bahati yao leo sikuvaa milipuko ningekufa nao. Duh! Kumbe wana bunduki. Acha nitoke nduki asije kunitarime.
Chanzo: Tanzania Daima Mei 25, 2011.

No comments: