The Chant of Savant

Thursday 9 June 2011

Bunge liwe linafanyika Railway Gerezani

BAADA ya kugundua uhovyo na uchovu wa wabunge wao wa ulaji, kijiwe kimekuja na mkakati wa kuwapindua ili walevi wapate wawakilishi wenye udhu na makali. Kuna kashfa zilizolazimisha kijiwe kuanza kufikiria kulipindua bunge.

Tunataka kurejesha heshima ya bunge na lenye viwango vya kistaarabu na si kuburuzana, kushindana kuonyesha fasheni za blackberry, dhahabu, mavazi na utumbo mwingine kama vile kulala bungeni, kupayuka na kupokea taarifa za wizi bila kuufanyia kazi.

Tunataka Bunge la walevi na si wachuma ngawira. Bunge tunalotaka si la kulipana posho za vikao na kupitisha miswaada na bajeti za kipuuzi. Hatutaki Bunge la jikoni bali la walevi.

Kwanza tulaani kitendo cha mandata kumkamata kiongozi wa upingaji bungeni bwana Freedom Mboe.

Geshi letu la mandata nalo limegeuzwa jibwa la Chama Cha Mafisadi kiasi kwa kuwa tayari kuwakamta wabunge huku likiwapigia saluti mafisadi. Acheni umbwa na unepi mtafanyiwa kitu mbaya siku moja. Shauri yenu.

Nashangaa. Kama Freedom angekuwa mbunge wa Chama Cha Magamba unadhani hao mbwa wa CCM, yaani Chama Cha Magamba wangethubutu kumkamata? Sijui kwanini hii mijitu haitaki kujifunza kutoka Misr!

Kuna siku hayo madaraka viraka yatachukuliwa na kupewa wengine. Yaani mauaji ya Talime hayajatulia mnakamata kiongozi wa upingaji. Kama hao wanaowatuma hawataki upinzani si watangaze ufalme ijulikane. Hayo ya kukamatwa wa arawa nayaachia hapa. pole sana arawa babangu.

Sababu ya pili ya kijiwe kudhamiria kutwaa Bunge ni ufisadi. Baada ya kuchunguza orodha ya wabunge na mishiko ya makali (sitting allowances) wanayopata bila kufanya lolote, kijiwe kimeamua tuchukue hatua. Tuhakikishe wabunge wote mafisi, mafisadi, magamba, vinyoka vilivyorithi nafasi za wazazi wao au kuukwaa kutokana na ukoo vipigwe kibuti.

Tatu, ni ubabe. Baada ya kuona mama Kipaza Sauti au microphone or speaker kwa kimombo kutembeza ubabe akitetea mafisadi waliomsimika, tumebuni mkakati wa kuhakikisha anapigwa chini kama alivyofanyiwa Sam Sixx kutokana na usongo wake wa kuwabamiza mafisadi.

Baada ya mama huyu aitwaye Annae Mwenye Makinda achezaye Makida makida kuwa mbabe na mroho na mbinafsi kiasi cha kufunga hata njia za watu ili ajenge hekalu lake, kijiwe kimeona ni busara kuanza mikakati ya kumgaragaza chini ili afanyiwe kweli kwa kumtosa.

Pia kijiwe kimegundua kuwa wabunge wanalipwa mishiko mikubwa ikilinganishwa na uchumi wa kaya. Hivyo, tumekuja na mkakati wa kupunguza maulaji yao kwa kuchagua watu wasio na stori na pesa wala utajiri bali uzalendo na maendeleo.

Nne, kashfa ya wengi wa wabunge kuwa vihiyo wenye shahada za kughusi imetulazimisha kuunda kamati ya muda au ad hoc committee ya kurejesha kaya kwenye mstari.

Tano, baada ya kuona mapapa na mabingwa wa ufisadi na ukoo na kujuana wakipewa uenyekiti wa kamati nyeti za Bunge, tumeamua kujipanga upya kulitwaa Bunge ili liwe na watu safi na si mafisi na mafisadi na magamba na vinyoka kama Jannie Makambale Mgosi, Hussain Muinyi, Emmy Nchimvi, Wars Kawaua na dada yake Zamazaradi.

Hapa bado hujawataja wengine wenye majina ya vigogo kama Msuuuya na wengine wengi wanaojulikana kuwapandikiza vitegemezi au wake zao bungeni. Wana kijiwe na walevi si wanafiki. Wanajua hata wakuu wa mawilaya hata mikowa walipewa ukuu kutokana na majina ya baba zao au kujipendekeza hata kujihonga kwao. Bado hapa hujaongelea wana geshi waliojazana kwenye vyeo vya kisiasa wakati ni kinyume cha sheria.

Sababu nyingine ya kuchukua hatua ni ile hali ya wabunge kushindwa kuliadhibu lisirikali tokana na kushindwa kulinda mali za walevi. Wako wapi akina Kagoda, EPA, SUKITA, Meremeta, IPTL, Richmond, Dowans na wengine wengi?

Ili kuhakikisha tunafanikiwa kuikomboa kaya kutoka kwenye mikono ya mafisi na mafisadi, tutaandaa mikutano kayani kote kutaka katiba ibadilishwe haraka na sifa za wagombea ubunge zibadilishwe. Tunapendekeza mgombea awe na sifa zifuatazo ili aweze kugombea ubunge.

Mosi, awe bingwa wa kupiga masumbwi na si kupika majungu wala kughushi vyeti kama wale walivyo. Pili, ajue kupayuka kwa sauti na busara kama mzee mwenyewe na si mipasho na umbea kama mgosi Machungi na Mape Nnaye.

Tatu, asiwe mpenzi wa njuluku kama Annae Makapi au Sisalama Kikwe ambao waliotumia kukuu kufanya umachinga kwa NGO.

Nne, awe tayari kuvua nguo si magamba. Maana uchafu wa mtu huonekana kwenye nguo kuliko ngozi ambayo hufichwa na hiyo nguo. Hivyo, tutapendekeza mwenye kutaka kuonyeshwa ukweli wa usafi wake avue nguo ili abaki utupu kila mtu aone madhambi yake.

Ewassa, Chwenge na Rostitamu mpo washirika? Stop cheating yourself just like the Bunge that plays bungee with the rights of our walevi. What a—lie so to speak.

Lol! Mwenembago kaishapanda kiasi cha kuanza kuongea kwa lugha ya majini ya kwa mama! Tuendelee na sifa za wabunge watarajiwa. Lazima mwenye kuutaka ubunge awe tayari kutangaza mali zake. Awe tayari kuchukia kitu kidogo na kikubwa yaani rushua.

Pia awe tayari kuvimbishwa mishavu kwa ngumi na asione aibu badala ya kuvimbisha matumbo na mishavu kwa pesa ya ufisadi. Aweze kuonea aibu kuvimbisha mitumbo na mishavu kwa pesa ya ufisadi.

Pia anapaswa ajue kuvaa gwanda au jezi ili awe tayari kupiga karate na si misuti ya ujambazi. Kwanza nani anataka suti Bongolalaland ambako joto ni kama tuko kwenye oveni? Nani anataka suti ili kumaliza kodi za walevi kwa kulipia viyoyozi kweni vya kwenye mashangingi yenu havitoshi?

Sifa nyingine, Kuwa tayari kutoa jasho kwa kukimbia ili kufanya mazoezi ya kuwachapa wapinzani wetu badala ya kukimbiza mishiko na dogo dogoz wakati wa vikao vya Bunge.

Pia mwanamume au mwanamke atakayeutaka ubunge awe tayari kuupenda udugu na si uheshimiwa wakati wengi wa wanaoung’ang’ania uheshimiwa hawana heshima wala kuistahili kutokana na matendo yao ya kinyani nyani. Hawa ni waishiwa.

Sifa nyingine ni ya Speaker. Lazima awe amesoma sheria, awe na mke au mume na si kanunga. Pia awe na akili timamu na busara na asipendekezwe kwa jinsia yake au ushikaji na mafisadi kama ilivyokuwa huko nyuma alipopigwa buti Sam Sixx.

Asiwe mbinafsi, mlazimishi, mpenda makuu wala tunda na chaguo la mafisadi. Aingie kwa sifa na si kubebwa na jinsia au kujuana.

Naona makabrasha ya kusaini mshiko yameletwa. Acha nijiwahi kutia mkono ili niende kuutwika na kusaka vyangu waliokuja kushiriki bunge la usiku kwenye nyumba za kulala wageni.

Bunge lifanyike uwanja wa ngumi Gerezani ili tuchapane ngumi sawa sawa.

Muishimiwa spika naomba kutoa hoja.

Chanzo:Tanzania Daima

1 comment:

Anonymous said...

nimependa sana hii mada kweli watu wanapenda uheshimiwa wakati ni waishiwa, maana hawa wabunge huku dodoma kaz yao kulala na wanafunzi wa cyuo vikuu na kuwaambukuza agonjwa siku zote za bunge wanachukua wanawake tofauti tena nasikia wengune wamewah kuua mwanafunz baada ya kugundua ana mwanaume mwingine me tanzania watu wana zid kuiharibu kwa matendo yao
.