The Chant of Savant

Sunday 18 March 2012

Arumeru wangemuuliza Mkapa Kiwira, EPA na NBC



Wengi Wanaojua madudu ya rais mstaafu Benjamin Mkapa walishangaa mantiki ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kumpa jukumu la kurejesha jimbo la Arumeru Mashariki baada ya kufariki kwa aliyekuwa mbunge wake. Kwa wanaojua jinsi Mkapa alivyomwangusha kipenzi chao Baba wa taifa mwalimu Julius Nyerere, walishangaa busara hii ya kumteua mtuhumiwa wa kufanya biashara ikulu, kuridhia ubinafsishaji wenye kila shaka, kujitwalia mali ya wananchi yaani mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira alioutwaa akiwa rais akishirikiana na waziri mwandamizi, familia zao na hata wakwe wa Mkapa. Hata hivyo habari zilizotufikia ni kwamba Mkapa amegwaya kwenda Arumeru Mashariki. Hili halituzuii kuuliza maswali ambayo angepambana nayo kule.
Wenye kumbukumbu na busara walishangaa kuteuliwa kushika usukani katika kampeni kwa mtu aliyewadhurumu wananchi benki yao ya biashara (NBC) iliyokuwa ikiingiza faida kuliko ilivyoelezewa. walishagaa mtu kama huyu aliyejenga msingi wa ufisadi na wizi wa wazi wazi unaoendelea kama kuingia mkataba wa hatari wa IPTL kupewa jukumu kubwa kama hili. Je huu si ushahidi kuwa CCM imeishiwa na kuparaganyika? Basi kwa niaba ya Mkapa iulizeni CCM itampelekea ujumbe wake. Je kule kutangaza mali zake wakati wa kuondoka madarakani kuliishia wapi? Muulize ni kwanini alibariki wizi wa pesa za umma chini ya ujambazi wa EPA ambapo mabilioni ya shilingi za wananchi yaliibiwa kugharimia uchaguzi wa aliyemfuatia ambaye naye, kama Mkapa, huwa hataki kujibu tuhuma. Endeleeni kumuuliza. Ni kwanini aliruhusu mkewe kujipatia utajiri wa haraka na haramu kupitia biashara ya NGO. Muulizeni ule uchumi wa kisasa alioahidi kwanini uligeuka uchumi wa kisasi na kifisadi. Muulizeni alikopata jeuri ya kujiuzia nyumba ya serikali na kuwapa marafiki zake nyumba nyingine. Muulize hata hayo mabilioni ya kujengea hekalu Mkuzi Lushoto yalitoka wapi?
Mngeweza kuendelea kumuuliza Mkapa hata CCM ni kwanini aliamua kukikabidhi chama cha wanyonge kwa mafisadi huku akiwaacha wakiwa yatima. Muulizeni ni kwanini ameendelea kunyamazia tuhuma zote zinazomkabili yeye, familia yake na marafiki zake? Je ataendelea kuishi kwa hisani ya Kikwete hadi lini? Kitu ambacho kiko wazi ni kwamba Mkapa hawezi kupata jibu lenye kuingilia akilini hata la swali moja. Sana sana akifika Arumeru Mashariki ataenda kupiga siasa za kukandiana na kujilisha pepo kuwa wapinzani hawana kitu wakati asiye na kitu ni yeye na chama chake ambacho kimeonyesha kuishiwa kulhali.
Kipindi hiki wananchi wa Arumeru Mashariki msikubali majungu naporojo za kwenye majukwaa bali muwape mtihani hao wanaotaka kuwawakilisha kuhakikisha wanaeleza na kuwahikikishia kuwa hawatakwenda kuwakilisha matumbo yao na koo zao hasa wale wanaoendekeza siasa za kurithishana kama ufalme.
Maswali mengine ya kumuuliza Mkapa ni kwanini chama chake na serikali yake wameamua kwa makusudi kutumia raslimali za umma kwa manufaa yao binafsi? Watu wa Arumeru Mashariki wanajua jinsi mbunga za wanyama zilizowazunguka zinavyonufaisha wageni na wenye madaraka wachache huku wanancni wakizidi kutopea kwenye umaskini wa kutengenezwa na waroho wachache wanaokaa ikulu kufanya biashara ya kujitwalia mali za umma. Hawa ni wezi wa kawaida hata kama wana madaraka. Hawa ni watu wa kuzomewa siyo kusikilizwa wala kushangiliwa. Kufanya hivyo ni kujidhalilisha hasa wananchi watakaotapeliwa na wezi wanaowajua fika. Je wananchi wa Arumeru Mashariki watajiruhusu kutumika kama daraja na ngazi ya watu waongo wachache kupandia kwenda kwenye neema itokanayo na kuwahujumu hao hao watakaopiga kura?
Kituko cha pili ni ubunge unaoanza kuwa wa kurithishana ambapo anayepeperusha bendera ya CCM ni mtoto wa aliyekuwa mbunge. Je tunaaza taratibu kujenga msingi wa siasa za kihindi? Hata hivyo, tujiulize, nani msafi kwa sasa anayeweza kuheshimika kwa wananchi ndani ya CCM baada ya wote kuchafuka au kuchafuana? Rejea kambi moja ya CCM hiyo hiyo iliyomtangaza mteule wa CCM Arumeru Mashariki kuwa si mtanzania. Leo uraia wake umepatikanaje haraka hivi?
Kama wananchi wa Arumeru Mashariki wanataka ukombozi na hawako tayari kutumiwa na wezi wenye madaraka basi wamuulize Mkapa swali moja kuu na la maana: ilikuwaje akajitwalia mali ya umma wakati alikuwa akituahidi kujenga uchumi imara ulioishia kuwa legelege?
Chanzo: Dira ya Mtanzania Machi, 2012

No comments: