The Chant of Savant

Thursday 31 May 2012

Hii sasa kaya ya madudu


BAADA ya kupata shahada zetu za udaktari, wana kijiwe tumeanza kuwa wachambuzi wa karibu kila jambo kuanzia majumbani mwetu hadi kijiweni.
Baada ya kuona jamaa zetu kule kwenye visiwa wameanzisha harakati za uangusho ili kuangusha kilicho halali, sisi tumeanzisha harakati za kuwaamsha walevi kuangusha kilicho haramu. Nadhani tunaelewana.
Leo uwanja ni wa Dk. Profesa Msomi Mkatataamaa ambaye tangu sasa tunamuita mpphilosophe. Mimi naitwa Guru of Philosophy au Abu Hekima kwa Kiarabu au baba wa maarifa kwa Kimakonde.
Kama nilivyogusia, kikao cha leo kitawaudhi wengi kutokana na Dk. Profesa M-philosophe kuahidi kuonyesha usomi wake katika kuchambua madudu ya kaya hii ambayo imeanza kugeuka kaya ya madudu.
Bila kupoteza muda anakohoa kidogo na kukwanyua mic, “Waheshimiwa madaktari na maprofesa wa kaya hii, nina furaha kubwa kuwapa mhadhara juu ya dhana nzima niliyojenga juu ya kaya yetu ambayo kusema ukweli imegeuka ya madudu.”
anainua kombe lake na kupiga tama na kuendelea, “Kwa sisi tuliosoma historia ya ukombozi kuanzia zama zile za Uamsho au Enlightment kwa lugha ya kikameruni, tunakumbuka jinsi mageuzi tunayofaidi leo yalivyoanzishwa na magwiji kama François-Marie Arouet de Voltaire, Lorenzo De Medici ambaye alisifika kuwa mtu wa kwanza kuwa tajiri duniani, John Locke, Sir Isaac Newton, Leonardo Da Vinci, Jean Jacques Rosseau, Montesqui, Thomas Hobbes na wengine wengi ambao nikiamua kuwataja tutakesha kabla ya kusikia ninachopanga kusema.”
Kabla ya kuendelea Dk. Maneno anachomekea: “Huyo Luhizo Medichi ndiyo nani tena? Nimependa jina lake maana ni kama la Kizigua.” Watu hawana mbavu.
Dk. Profesa Msomi Mphilosophe anajibu: “Wala huyu jamaa siyo Luhizo wala si mzigua bali muitaliano aliyeanzisha mageuzi ya biashara kwa kuchuma pesa nyingi na kudhamini vikao vingi vya kupinga kanisa la Kirumi na serikali kutokana na uchakavu wake hasa ufisadi kama huu mnaoona leo. Kwa ufupi ni kwamba jamaa huyu na wenzake walikuwa wakikutana kwenye vijiwe kama sisi. Tofauti ni kwamba wao waliviita vijiwe vyao salon.”
Kabla ya kuendelea Dk. Mgosi Machungi anakwanyua mic. “Mgoshi, mie sikueewi hasa unaposema eti Uhizo si Mzigua.”
Msomi Mphilosophe anamkosoa Dk. Mgosi Machungi: “Sijakana kuwa Luhizo si Mzigua. nilichosema ni kwamba De Medici si Mzigua bali mtaliana. Hata hivyo hilo si tatizo. nitakupa mfano mwingine, hivi nikisema kuwa Rostitamu si fisadi tutakubaliana? Nikisema jamaa huyu mtaalamu wa madudu anayemwendesha Njaa Kaya ni bingwa madudu anayesukumwa na kukosa uzalendo kutokana kutokuwa raia wa kaya hii nitakosea?”
Anakunywa kahawa na kuendelea: “Kwa taarifa yako Dk. Mgosi kuna wengi nimewasaza ambao wangekuchanganya kiasi cha kuona kuwa ni Wasambaa. Niwape mfano, kuna magwiji kama Ulrich Zwingli, Barthasar Hubmaier, Conrad Grebbe, Martin Luther, John Kalvin na wengine wengi. Kwa vile leo mada yangu ni madudu ya kaya, naona niwape fursa nanyi mtoe mawazo yenu kuhusiana na huu uoza na madudu ambayo waziri mmoja Nshomile alisema aliyekuta kwenye idara ya Mali ya Siri.”
“Ahaa kumbe! Kumbe ulikuwa unaelekea huko! Sasa nimekupata,” alisema Dk. Mipawa na kuendelea: “Mwenzenu nimeogopa ingawa nimefurahi kujua siri ya utajiri wa jamaa zangu wanaofanya kazi kule Mali ya Siri kama msukuma mwenzangu Heze Maige. kwa taarifa yenu ni kwamba kaya inaliwa mchana kweupe?”
Anavuta kipisi chake cha sigara kali na kumpasia Dk. Mbwa Mwitu na kuendelea, “Jamaa kwa kuchukua mabibi utadhani Liumba! Jamaa wana jeuri ya pesa usiambiwe. kwa sasa wana uwezo hata wa kuwanunua wakubwa na kuendelea kupeta kinamna. Nyie ngoje muone. Baada ya wezi wa miwa kumtimua unadhani atasota kama wengi wanavyodhani? Atateuliwa ubalozi kama yule Daktari Ladi Komba wa kwa M7 au daktari feki Nshomile Kamalae,”
Kabla ya kuendelea, Dk. Mchunguliaje anachomekea: “Kwanini asiende nje kuula na kuhakikisha wale wanyama aliowasafirisha wanazaliana na kuzuia watalii kuja kwetu? Kwa taarifa yenu, kama alivyosema mpayukaji mmoja kuwa biashara ya bwimbwi inafanywa na wakubwa, ukweli ni kwamba Maige hakusafirisha wanyama peke yake. Huu ni mtandao. Habari hizi nilipewa na jamaa yangu anayefanya kazi usalama wa taifa.”
Naona kila mtu anamuangalia mwenzake kuona jinsi ya kumeza kirungu hiki.
Dk. Mpemba naye hataki kujivunga anakwanyua mic: “Yakhe mie nshashuhudia kitoto kichanga tena cha Jana kiniofanya kazi pale Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere kikinunua viwanja na upuuzi mwingine karibu kula mahali. Nasikia eti hawa mafisadi wadogo wala na wakubwa na wakubwa wana kula na wakubwa hadi mkubwa.”
Dk. Mpemba umeniacha hoi anasema, Dk. Kidevu. “Yaani unataka kuniambia kuwa na mkubwa yumo kwenye dili hili? Kweli kama alivyosema Dk. Profesa Mphilisophe hii kaya ya madudu. hapa hujagusia watoto wao na wake zao ambao nao wamegeuka wakubwa nyuma ya pazia.”
Dk. Mpemba anaendelea: “Yakhe nimesikia kuwawana akaunti nje ya nchi na waendapo huko kuongeza pesa waenda na machangudoa wengi kama njugu. Nakumbuka, kimada wa kijana anayesimamia meta ya mafuta kule kwa akina waja leo warudi nasikia ana pesa kiasi cha kumnunulia gari kila mwanamke anayetembea naye. Hivyo kaya yetu si masikini bali haya hawa wadudu wanainyevuanyevua.”
Watu hawana mbavu. Tukiwa tunacheka Dk. Mbwa Mwitu anauliza: “Ami hebu njuze, wainyevuanyevua kaya wapi?” Anauliza kwa lafudhi ya Kipemba.
Dk. Mpemba hajali anajibu: “Wainyevua kote. hebu nenda pale banki kuu, uwanja wa ndege, Uhamiaji, mbuga za wanyama, bandari, Madini, Viwanda, Elimu, Mitaani, Polisi, Mamlaka ya Mapato ambayo yageuka sasa Mamlaka ya Mapoteo na kwingineko kwingi uone. Watu waiba kana kwamba kaya hii ya vichaa au haina mwenye Wallahi.”
Tukiwa tunaendelea kutongoa falsafa si likapita jina la kijana mmoja mdogo anayefanya kazi TRA. Gari lenyewe ni aina ya Buggarti. Kila mtu anashangaa kiasi cha inzi kujaa kwenye kahawa zetu.
Kama imekugusa tusameheane.
Acha nijikate nikatafute unga wa bibi mkubwa.
Chanzo: Tanzania Daima Mei 30, 2012.

No comments: