The Chant of Savant

Wednesday 23 May 2012

Kuanzia leo ndata bila cheti hanikamati


LEO wanywa kahawa wamejilawa kweli kweli kutokana na kuwapo tukio muhimu kwa kijiwe. Kusema ukweli leo ni siku muhimu na ya kukumbukwa kwani ni siku ya kutunukiwa udaktari kwa wanakijiwe uliotolewa na chuo kimoja nchini, jina kapuni.
Samahani kwa kuficha jina la chuo kilichotunikia kijiwe kizima PhD ni kutokana na kuogopa wapenda udaktari wasifurike kule kughushi. Ila msomaji ujue kuwa chuo hiki ni genuine na tuliopewa hatujajikomba wala kuhonga tupewa shahada hii inayopagawisha wabongoalalalanders na wadanganyika hasa wenye nazo na madaraka.
Kutokana na kupewa shahada za udaktari, madaktari wapya leo watajadili aibu ya ndata na wasoja kughushi vyeti vya taaluma kama wale mawaziri wa Njaa Kaya ambao ameamua kufa nao kutokana na huduma safi ya kuibia kaya wanayompa. Hayo tuyaache. Leo ni sisi na ndata na ndata nasi kutokana na wanavyotuhangaisha kwa kutukamata tukiwa tunarejea toka kijiweni ukiachia mbali kuingilia mada zetu kila mara hasa tunapogusa wezi wenye madaraka.
Kama kawa Dk. Mgosi Machungi analianzisha. “Wagosi, mie sieewi hii kaya inapeekwa wapi?”
Kabla ya kumaliza Dk Mchunguliaji anadandia, “Kwani hujui kuwa inapelekwa jehanamu au nalo hili uliongoja kulijua ulipopewe shahada kuu?”
Dk. Mgosi Machungi hakupenda alivyojibiwa kwa kuonyeshwa kama hajaenda shule. anakula mic kwa hasira, “Daktai Mchunguliaji tiheshimiane nisijepiga mtu zongo bure. Nauiza swai ya maana wewe unaanga nkungukwa!”
Dk. Mchunguliaji anaomba radhi na kikao kinaendelea ambapo pia anakatua mic, “Madaktari watukufu wasomi wa kaya na kijiwe hiki, kwanza nawapongezeni kwa kupewa zana zetu za ulaji hasa huko nje ambako kila mtu anapagawishwa na udaktari. Hata hivyo udaktari tuliopewa si wa kutibu watu. Hivyo jihadharini msijeletewa wagonjwa mkaaibika.”
Kabla ya kuendelea Dk. Mipawa anakula mic, “Mie nikiletewa mgonjwa namtibu. Kwani kazi? Si unamuandikia karatasi kwenda kununua dawa kwenye duka la madawa na anakulipa pesa ya kumuona daktari.”
Kijiwe hakina mbavu kutokana na Dk Mipawa anavyoonyesha makali yake.
Tukiwa tunaangua kicheko si Dk. Mbwa Mwitu aliingia akiwa na gazeti la Tanzania Daima. Anasema bila hata kutuamkua, “Jamani waheshimiwa,” Kabla ya kuendelea, Dk Eng. Maneno anadakia na kusema, “Sisi si waheshimiwa tena bali madaktari. Omba radhi uendelee kutupa ulilo nalo moyoni.”
Dk Mbwa Mwitu anaomba radhi na kusema, “Wenzangu nisameheni. mwajua kuwa cheo hiki bado ni kipya hivyo nilisahau. Nisameheni.” Anaendelea, huku akiwa anabwaga gazeti mezani huku kila mtu akiligombea asome kwanza. “Mmeona huu upuuzi unaofanywa na lisirikali na makuwadi wake? Eti ndata 4,000 na masoja 2,000 wamepatikana na kashfa ya kughushi!”
Dk. Kidevu hangoji hata aendelee, anakatua mic, “Unashangaa la ndata kughushi wakati mawaziri wameghushi na hakuna anayewashughulikia. Usishangae siku moja ukiambiwa hata Njaa Kaya alighushi kutokana na elimu na matendo yake kuwa mazabe matupu.”
Dk. Mpemba hajivungi, anakatua mic, “Siye Pemba tushazoea haya mambo. Mwankumbuka yule komandoo alokuwa akitutesa?” Anakatua kashata na kuendelea, “Yu aitwa daktari wakati hata hicho cheti cha fomu foo hana!”
Hatuna mbavu tokana na Mpemba anavyokamua lafudhi ya Kipemba. Wakati tukiendelea kucheka, Dk. Eng. Maneno anakamua mic, “Yule jamaa laana tupu. nasikia siku hizi hasikii kabisa.”
Dk Mpemba anaramba tena mic, “Kweli hasikii tena. hata wale walokuwa wakintumia weshankimbia yu ahangaika kama ndege alonaswa ntegoni. Hizo laana wallahi. Hata hawa waloghushi huku wakikamata wenzao watajalaaniwa wallahi.”
Nami Profesa Dk. Mpayukaji naingilia kati baada ya kukaa muda mrefu. Nakula mic, “Hapa laana siyo hawa wanaoghushi basi mfumo na wale wanaowafuga. Kweli kaya imegeuka kaya ya matapeli. Usishangae siku moja kusikia Dk. Koplo Mwita. Dk. Sajenti Chacha. Dk. Afande Ulaji na Dk. Mgambo wa Jiji, Dk. Mpigadebe na Dk. Masaburi, Dk. Mamantilie na kadhalika.”
Watu hatuna mbavu tena. Profesa Dk. Msomi Mkatatamaa anavaa jezi na kuingia uwanjani. Maana kabla mimi na yeye hatujaongea kijiwe huwa kinahisi kama hakujafanyika kitu.
Anakula mic huku akijifuta mdomo baada ya kunywa kahawa yake, “Wapendwa madaktari na wana taaluma wa kweli, kwanza nawapongeza kwa kupata nondo hii muhimu inayowavua nguo watu wengi wenye majina yao.”
Kabla ya kuendelea anajaribu kufukuza moshi wa sigara kali unaovurumishwa na Dk. Kidevu ambaye ametoka kubomu kipisi kwa Dk. Mbwa Mwitu.
Profesa Dk. Msomi anaendelea, “Hapa tusilaumu watu binfsi bali jamii hasa kaya nzima. Kama alivyosema profesa Dk Mpayukaji mwenzangu kuwa tatizo hapa ni mfumo, pia tatizo ni wana jamii wenyewe wanaokubali kuliwa na kuchakachuliwa kila uchao.”
Kabla ya kuendelea, Dk. Mgosi Machungi anamkatisha, “Profesa Daktai Msomi tiombe radhi kwa kusema eti tinaliwa na kuchakachuiwa. Sema wao wanachakachuana isipokuwa sisi wazee wa kijiwe. Vinginevyo unatitukana wote.”
Profesa Dk Msomi anaendelea, “Na iwe hivyo Dk. Mgosi. Sisi hatuwezi kuchakachuliwa wala kuliwa. Hamuoni tulivyopata shahada hizi nzito bila umaarufu wowote wala kutembeza pesa. Sisi ndiyo hazina ya ubongo ya kaya nzima hata rahisi anajua hili. Hivyo, ninachomaanisha ni kwamba kama wanakaya wataendelea kuvumilia uchafu ambapo mtu mchafu anamkamata mtu msafi, watakuja kufanyiwa kitu mbaya siku moja wasilalamike.”
Anavuta kombe lake na kupiga tama mbili na kuendelea, “Kimsingi kaya yetu imeingiliwa na mchezo mchafu ambapo wakubwa wamewageuza wanakaya punda wa kubeba upuuzi wao. Kuanzia leo sitaruhusu polisi anikamate au kunihoji bila kuonyesha vyeti vyake. Nina mpango wa kumwandikia rahisi na spika wa Bunge barua waitishe bunge na kutunga sheria inayomtaka kila askari kuwa na vyeti vyake kila anapokuwa.”
Kabla ya kuendelea Dk Mipawa anaingilia kati, “Kaka hilo halitasaidia. utajuaje kama vyeti watakavyokuwa navyo havijakachuliwa? Watu wanachakachua kura washindwe vyeti? Wanachakachua hata noti zetu tena mle mle banki, washindwe vyeti?”
Profesa Dk. Msomi anaonekana kukubaliana na hoja ya Dk. Mipawa. Anauliza kwa mshangao, “Sasa tufanyeje?”
Dk. Mipawa anajibu haraka, “Tufanye kama Uchina. Tukimshika mtu na cheti cha kughushi, au akifanya ufisadi tunanyongelea mbali.”
Dk. Eng. Maneno anaingilia, “Sasa hapa kaka umegusa pabaya. Utanyongwa wewe. Kambale wote wana ndevu. Naona ndata wanakuja na mikwara yao. Acha tuwazomee kwa kughushi vyeti.
Chanzo: Tanzania Daima Mei 23, 2012.

No comments: