The Chant of Savant

Wednesday 23 January 2013

Kikwete tunataka matendo si maneno



Hivi karibuni rais Jakaya Kikwete alikaririwa akisema kuwa uvumilivu sasa kwisha. Alisema, “Serikali haitavumilia vurugu wala ukabila kwa namna yoyote ile…. Mwaka 2012 vurugu zenye sura ya kidini zilianza kujitokeza ila sasa nasema kwamba hatutazivumilia kwa namna yeyote ile, inatosha,” Je Kikwete amekumbuka blanketi asubuhi? Je uzoefu wa kufanya mambo wa Kikwete unasemaje? Je Kikwete anasogeza muda ili amalize ngwe yake na kuliacha tatizo pale pale kama ambavyo amefanya kwa matatizo mengine kuanzia ufisadi, ujambazi, kuporomoka uchumi, muungano, udini, ukabila, ukanda, mitandao kwenye chama chake na mengine mengi?
Ni kweli kuwa mwaka jana taifa letu liligeuka gumzo kimataifa baada ya chomaji makanisa uliotokea baada ya watoto kufanya utoto kutokana na kufundishwa imani potofu na za kishirikina.
Je baada ya haya kutokea serikali ilifanya nini cha mno iwapo vyanzo vya kadhia hii yaani mihadhara inayoendeshwa na watu wasio na taaluma si ya kidunia wala ya kidini imepigwa marufuku zaidi ya kushamiri?
Leo tunajua fika kuwa Kikwete hajasukumwa na dhamira ya kutatua haya matatizo ya udini na ukanda bali kutaka kuingiza kipato kitokanacho na kuuza gesi ya Msimbati. Hii ni baada ya watu wa Mtwara kuja na hoja kuwa lazima gesi iwanufaishe wao kwanza na miundo mbinu yote lazima ijengwe Mtwara. je watu wa Mtwara wanaohofia nini zaidi ya ufisadi na upendeleo? Je Kikwete katika maelezo yake ametoa majibu ya tatizo hili yanayoingia akilini? Nadhani watu wa Mtwara wanajua ujambazi wa Richmond, Dowans na mwingine unaohusisha nishati. Pia wanajua udhaifu wa serikali ambayo kimsingi, kuna dhana imejengeka kuwa imo mikononi mwa mafisadi ambao Kikwete aliwahi kukiri kuwa na orodha yao na asiwaghulikie kwa sababu ajuazo.
Hebu tuangalie nukuu nyingine ya Kikwete, “Unawezaje kuwa na nchi moja na taifa moja wakati kila mmoja anadai rasilimali kutoka kwenye eneo moja ibakie na kunufaisha watu wa eneo hilo tu. Huwezi kuwa na nchi moja na yenye umoja wakati kuna nchi ya gesi asilia kule Mtwara, kuna nchi ya kahawa kule Kilimanjaro, kuna nchi ya chai na ndizi kule Bukoba,”
Kama inawezekana kuwa na watanzania walio juu ya sheria na wale ambao wako chini ya sheria lolote lawezekana. Watanzania si wajinga kiasi hiki. Kikwete anapaswa aambiwe ukweli kuwa hawezi kueleweka kwa vile amekuwa mfadhili na muhimili mkubwa wa haya madudu. Kama watu wanaona jinsi pesa inavyoibiwa na watu walio karibu na rais na rais hachukui hatua unadhani watamwamini? Hivi nani asiyejua kuwa Richmond iliyoingizwa na swahiba mkuu wa Kikwete, Edward Lowassa ililiweka taifa msambweni kiuchumi? Je Kikwete amefanya nini kuonyesha uongozi na uwajibikaji? Nani hajui sakata la rais mstaafu Benjamin Mkapa mkewe watoto wake na wakwe zake kujitwalia migodi ya makaa ya Kiwira huku Kikwete akiulizwa atachukua hatua gani anajibu” Mwacheni mzee Mkapa apumzike. Wananchi wa Mtwara hawako tayari kuona gesi yao inabinafsishwa ima kwa Kikwete au marafiki zake? Kumbuka ni kusini huko huko walioanzisha vita ya maji maji wakati wengine walikuwa wakigwaya. Wanajua wanachotaka na jinsi ya kukipata. Hivyo, dawa si kuwatisha wala kuwaongopea. Wanajua kuwa sekta ya nishati ndiyo inayoongoza kwa ufisadi na kutoa kipato kwa mafisadi. Wanajua kuwa Tanesco haikubinafishwa kwa vile ilikuwa haiwezi kujiendesha bali uroho na upogo wa watawala. Wanajua kuwa mgao na ulanguzi wa umeme vimesababishwa na ufisadi unaolindwa na kutendwa na watawala na mawakala wao. Wanajua kila kitu.
Wamajua kuwa Kikwete anawadanganya na hana nia ya kufanya lolote kwa faida yao. Wanajua kuwa hata mwaka 2006 alipowaambia kuwa ana orodha ya mafisadi, majambazi na wauza unga na asiwashughulikie ilikuwa ni danganya toto. Hapa hakuna cha kugawa nchi wala nini? Kama ufisadi umeigawa nchi kwanini gesi ya Msimbati iwe tatizo?
Si uzushi wala upendeleo kusema kuwa serikali yetu imefuga hisia za udini, ukabila, ufisadi, ukanda na hata mitandao nchini mwetu. Maana kumekuwa na watu wanaoota ndoto za mchana kuwa kuna siku Tanzania itatawaliwa kaiislam au kikiristo au kikanda au kikabila. Ila wanasahau kuwa uislam haujawahi kutawala popote ukiachia mbali baadhi ya watawala kuutumia kufikia malengo yao. Mfalme Constantine aliutumia Ukristo kutawala Rumi, Ezana (Kush) huku watawala wa Ottoman, Mughal na Safavid nao wakiutumia uislam kujiimarisha kwenye madaraka. Kuna watu wanaoota kuwa juu ya sheria wakifaidi keki ya taifa huku wengine wakifa njaa.
Kinachofanya serikali ilaumiwe ni ile hali ya kuruhusu kila mtu kujifanyia atakavyo bila kufuata sheria. kwa mfano, madhehebu ya dini yalipaswa kusajili kwa sharti kuwa yakienda kinyume na matarajio ya serikali yanafutiliwa mbali. Leo tuna maaskofu wengi feki wanaotumia dini kuwaibia maskini na kuwadanganya. Wanazuka k ila uchao. Tuna mashehe wengi wanaoibuka na kutangaza vitu vya ajabu kama hawa wanaotaka kuangusha Bakwata au kutaka kueneza uislam wa kihafidhina ambao hata mtume hakuuacha.
Hata hivyo, inapaswa watu wa namna hii kuambiwa kuwa tulipopigania uhuru tulipigania uhuru kama watanzania na si waislam wala wakristo, wamakonde, wana CCM na upuuzi mwingine. Mtu yeyeto aweza kuingia dini yoyote na kutoka lakini hawezi kufanya hivyo kwa uraia wake kirahisi hivyo. Kwenye kujiunga na dini hakuna maombi wala masharti sawa na uraia. Mbona wakati tukiingizwa kwenye mfumo wa kikoloni au kupelekwa utumwani hizi dini zinazotaka mamlaka leo hazikutusaidia zaidi ya kuwa wakala wa mateso yetu? Kuna haja ya kusoma historia kuepuka aibu ya kiakili kama hii. Hivyo, hawa al muthnaka wanaoota mchana kudhani Tanzania inaweza kutawaliwa kidini, washikishwe adabu mara moja.
Tumalizie na kadhia ya gesi asili Mtwara. Serikali isiposhughulikia ufisadi na ubaguzi wa kimaeneo yatatokea mengi kama hili la Mtwara. Jibu si kuwatisha watu wa Mtwara bali kuwatendea haki sawa na watanzania wengine.
Chanzo: Tanzania Daima Januari 23, 2013.

No comments: