The Chant of Savant

Tuesday 25 June 2013

Kijiwe charejea toka vakesheni


SAFU hii inawaleteeni habari njema sana ya ukombozi. Ni kuhusu kumalizika kwa vakesheni ya wanakijiwe ya miezi sita.
Wapenzi wetu walituandikia e-mails wakidhani tumededishwa na mibomu ya Arusha iliyorushwa na magaidi na washenzi wasio na maana.
Hivyo, tulikuta kijiwe kimejaa vumbi. Si unaona kijiweni palivyojaa vumbi? Tunakumbuka ujumbe wa wasiwasi juu ya uhai wa troupe yetu iliyotoka kwa Sheddy Mijjinga wa kule Mza. Hatuwezi kutaja wote waliojali ila tunawashukuru.
Tumerejea kwa kasi mpya, nguvu mpya na ari mpya, si ya kufanya ufisadi na usanii, bali kuendeleza libeneke ya ukombozi. Tulikwenda vakesheni kutokana na sababu nyingi.
Mosi, kupumzika baada ya kutumikia kijiwe tangu tuliposhinda uchaguzi bila kuchakachua wala mizengwe. Hatukuwa tumepumzika wala kufanya ziara yoyote nje, ukiachia mbali mkiti kwenda kwenye kutoa ushauri kule Masri na Libya wakati wa kitimtim kilichowahenyesha wahuni, kilichomnyima wibari mkia. Pia nilikwenda Kenya kusimamia uchakachuzi uliofanyika Machi 5 ambako Moyi Kibaka aliiba kura na kumpa mkyuki mwenzake Uhuruto.
Pili, tulipata wivu (si wa kike) baada ya kuona mkuu, bi mkubwa wake na waramba viatu wakizurura mara kwa mara kwa njuluku za walevi bila kufanya kazi pevu kama yetu.  Tuliona lau twende kule kuangalia mambo ya maana ili tukirejea tuyafanye kayani na kijiweni.
Mwenzenu nilikuwa sijaenda kuangalia mechi dimbani kwa miaka mingi. Hivyo nilikwenda kwa mama kuona timu kama Asenali, Manchesta, Sandaland na nyingine lau kupata jezi na picha za ukumbusho.
Bi mkubwa wangu naye alipewa tuzo ya kuwatumia wake wa walevi chini ya asasi yake ya Maulaji ya Wake wa Wakubwa (MAWAWA) na kujitengenezea pesa haraka huku watasha wasimstukie. Alikuwa kule kwa Joji Kichaka kuipokea japo sikuhudhuria baada ya kukosana nilipomshauri kwenye kuipokea aongee kimakonde na si kimombo kutokana na kumpiga chenga na kupandisha pressure anapokiongea. Nilihofia angeweza kudedi mbele zangu.
Wakati nikitanua kule New York, Mgosi Machungi alikuwa zake kwa akina Aloha kule Hawaii alikozaliwa Obamiza akipigiwa kifaa kiitwacho ukulele (si kelele ya uswazi). Good news, Mgosi Machungi alibarikiwa kupata mtoto wa kiume aitwaye Shenkhondo. Baada ya bi mkubwa wake Nesaa kujifungua tulikwenda zetu Sauzi kumjulia hali Diba wa Madiba.
Wengine walienda wapi?  Siri kubwa maana walikwenda kujifunza jinsi ya kupiga mtu chini, hasa anapochukua ulaji na kufanya ufisadi badala ya kuwatumikia walevi. Isitoshe tumefanya siri ili magaidi ya kindata yasiwafuatilie na kujua siri zao za kupambana na ugaidi wao na kuanza kuwamiminia risasi.
Kwa vile tulikuwa vakesheni kwa muda mrefu, tumekuta viporo vingi mezani. Kama miezi sita imekuwa hivi, hawa wazururaji wenu ambao kila siku kiguu na njia wataacha viporo kiasi gani kukuuu?
Leo kikao chetu ni cha laana. Tunalaani kwa nguvu zote unyama, uhuni na ushenzi ulioanza kuwa mazoea kama vile kumteka Abusalomu Kijumba. Tunalaani vipigo na uhuni uliofanyika Ntwara kuwazuia walevi wasidai wese lao lisichezewe na mafisadi waliokwishaleta makampuni yao kujenga mibomba ya kukamulia wese.
Tatu, tunalaani mauaji na ugaidi vilivyofanyika Soweto Arusha baada ya magaidindata kushambulia mkutano wa Chakudema huku wakitumia mibunduki kumiminia watu shaba.
Nne, tunalaani ufisadi uliowezesha kujengwa mghorofa wa Ugabacholini ambao uliangukia walevi kibao huku uliobakia ukiendelea kupigwa danadana na mafwisadi wanaolinda ulaji wao.
Tano, tunalaani matamshi ya kishetani na kishenzi yaliyotolewa na wapauuzi fulani wakidai Chakudema eti imejilipua kutaka huruma ya walevi. Hawa walipaswa kuchomwa moto kama vibaka.
Nani mara hii anaweza kuacha kulaani mafyatu kama vile Mizengwe Pindua ambaye amepinda kwelikweli, Nipe Mapepe Ninaye, Mwingurumbili Michembe na Mchunga Kondoo Mtukula? Shame on you goons Ukiondoa Pindua hatukushangaa kusikia vihiyo hawa walioghushi na tapeli aliyejipachika uchunga wakipayuka kwa vile wanathibitisha walivyo matapeli na vihiyo wa kutupwa.
Sita, tunalaani lijibajeti la kijambazi ambapo njuluku nyingi inatengwa kwa shughuli za matanuzi ya wazururaji huku walevi wakiendelea kuumia na kunyotoka roho.
Hivi huyu jamaa tunayeambiwa ni profwesa mbona haonyeshi uprofwesa wake au ni yale yale ya akina J4 Magimbe na wenzake wanaoboronga kila uchao?
Baadhi ya maprofwesa wa Kibongo hovyo kabisa. Hebu muangalie bi mkubwa Anna Kajumuzi Tibainjuke anavyoendelea kuaibika baada ya magabacholi kumzidi kete pamoja na kutangaza ataporomosha mjengo asijue ataporomoka yeye Saba, tunalaani ufisadi wa J4 Kawa-Dog aliyefelisha watoto wa walevi akaendelea kukataa kuachia ngazi.
Tunamlaani hata aliyemteua na kuendelea kumvumilia kwa vile wanatoka kaya moja.  Hakuna Kawa-Dog alipotuacha hoi kama kufuta matokeo ya fomu foo na baadaye kuyarejesha kwa kuwapa ushindi waliosemekana kushindwa. Hivi hapa kihiyo kati ya watoto wa fomu foo failure na Kawa-Dog ni nani?
Nane, tunalaani kitendo cha mkuu mwenyewe kuendelea kutanua kwa Mother akijinoma na timu za uchochoroni za huko, huku walevi wakiendelea kunyotolewa roho na watu wake. This is very serious. Hata hivyo, hatuna wasi wasi. Maana msomi Mkatatamaa kwenye vakesheni yake alikuwa The Hague akiangalia uwezekano wa wahuni hawa kufikishwa kule na kunyea debe.
Hata kwenye kikao changu na Bani Kii Mwezi, katibu mkuu wa YUNO tuliongelea suala hili alipokuwa akinipa michapo juu ya yule mama aliyempa ulaji akaenda pale kuonyesha ushamba wake hatimaye akamtimua na kurejea kwenye genge lake la ulaji ambalo lilimpa ulaji uchwara.
Sina haja ya kumficha kwa vile mnamfahamu kuwa ni   Dakitari Acha Rozi Migiroo. Bwana Bani Kii Mwezi aliniomba nikubali aniteue kurejesha heshima ya kaya nikakataa kwa vile kazi ya kukomboa walevi ni kubwa na ngumu na nyeti kuliko hiyo aliyotaka niifanye.
Hakuna kitu kilimsononesha kama kumpa skandali ya mama mmoja jambazi aliyewahi kupewa uwakilishaji kwa Joji Kichaka na kwa Mother wakati alikuwa mwezeshaji wa ujambazi wa HEPA. Nadhani mwamjua. Ni Mwanawaidd Maajari.
Naona wale ndata wameshika kitu kama bomu. Acha niishie kabla hawajanilipua bure na kusema nimejilipua mwenyewe wakati bado ugali mtamu.
Chanzo: Tanzania Daima Juni 26, 2013.

No comments: