The Chant of Savant

Saturday 3 May 2014

Katiba mpya: Mikakati ya mlevi kuchanga njuluku

         Baada ya kutoa lecture ya kuua mtu kule Dodoma na kugundua kuwa hakikueleweka mlevi hajakata tamaa sawa na Njaa Kaya ambaye hajakata tamaa kuvuruga. Nilijitahidi kutumia usomi wangu wa Constitutional Law kuwaonyesha walevi njia bila mafanikio. Kuna kipindi nilishauriwa nitumie ujuzi wangu kama yule profesa kidhabu aliyeonyesha kulalia upande wa Chama twawala bila aibu asijue maandiko yake ya awali yangemsuta. Hata hivyo, mchoyo hana maadili zaidi ya madili. Profesa Shivieji upo mwanangu? Acha hizo. Usomi si ukahaba wa kutumiwa na kila mwenye njuluku.
 Katika mhadhara wangu nilipendekeza wavunje muungano. Baada ya kuona kuwa hili nalo halieleweki naanza kupanga kwenda kule kupiga njuluku. Tofauti na Shivijie, natangaza wazi kuwa nakwenda kule kupiga njuluku au vipi? Sitajificha kwenye vitabu wala kuwa tayari kutumiwa na washenzi waliochoka na kuchakaa waking’ang’ania upuuzi wa utitiri wa ulaji. Sera yangu inafahamika kuwa ni siri tena kali moja. Mbili au tatu ni wizi mtupu na kuwatwisha walevi mzito unaonuka wa walaji.
Baada ya kugundua kuwa mtu anaweza kuchanga njuluku kirahisi kwenye Bunge la ulaji la Katiba, nimeamua kusukuti kutia timu lau nami nizoea kama wale mabambataa na mavuvuzela mabingwa wa mitusi na mipasho. Ngoja nifanya mazoezi ya kupasha na kumwaga radhi.
Nikifika naanza, “Wewe unayenamba niufyate kamwambie mama yako. Mie nshaufyatua kwa sana. Nimeishazalishwa sorry zaa vitegemezi kibao. Halafu waone wale wanaojifanya kupinga. Mbona hampingi mshiko? Macho ka nyau. Vous etes imbeciles comment les vaches et les camions et les escargots et quelque chose dans le pays. Vous etes les voleurs politique que je vais frapper moi-meme.” Nikiangusha hii mitusi ya kifaransa watakoma na kunipa uchache wangu na kuniona bonge la mwanasiasa si haba. Mitusi na mipasho yangu itapata soko hasa pale wakubwa watakavyoishabikia kana kwamba ni kitu chema. Hapa nadhani nitapata ujiko kama Mr F*ck you aka Pita Serukamba. Hapa bila shaka vijembe vyangu vitatumika kama vishoka vya kukata njuluku. Kama vishoka wanaweza kuwaibia watu kwa kuwaunganisha umeme kinyemela kwanini nami nisitumie vijembe vyangu kugema njuluku?
Ujuzi wangu wa utafiti unaniambia kuwa katika ulaji huu uhitaji kufikiri wala kufanya lolote zaidi ya kupayuka na kumwaga mitusi mizito mizito huku povu na jasho vikikutoka kuonyesha uzalendo. Ukiona mitusi imekwama una-Lukuvi kidogo. Unajua maana yaku-Lukuvi? Simple, unaunda urongo na vitisho tena unakwenda mtaani au matanga na kuvimwaga kule halafu unajiondokea.  Siku hizi mitusi, vitisho na mipasho vinalipa kuliko hata taarabu. Uhitaji wapiga gitaa wala vyombo vya muziki zaidi ya wapiga meza wakikushangilia kila unapochafua hewa kwa midomo yako.
Kitu kingine ambacho wachovu hawajanyaka ni ukweli kuwa posho za makalio zilizokuwa zimepigwa marufuku mjengoni zimerejea kwa mlango wa nyuma. Hebu fikiria. Wale wanaolipwa kwa kushangilia mipasho na mitusi wanalipwa kwa sababu gani zaidi ya kukaa kwenye makochi tena ya bei mbaya mjengoni? Hapa ni ligi ya ulaji. Wanamipasho na matusi wanalipwa kwa kugeuza midomo yao makalio na kuchafua hewa huku washangaliaji wao wakilipwa posho ya makalio tuseme na makoo yanayotumiwa kuzomea wenzao.
Kitu kingine ambacho nimegundua kuwa kinalipa njengoni ni fitina. Ukiwa bingwa wa kutengeneza fitina na ugogoro lazima utaondoka na uchache bila hata kutoa jasho. Unaweza kuzusha kuwa umegundua kuwa kuna mataifa ya nje yanaingilia mchakato wa Katiba. Tena unaapa kwa jina la bibi wa bibi wa nyanya ya shangazi yako kuwa umekamata waraka maalumu wa kutekeleza hili. Ukiona hakieleweki unaapa kwa kuramba pua yako ili kuonyesha kuwa huongopi na siku zinakwenda huku njuluku zikiingia. Mbinu hii kwa kinyasa huitwa delaying technique aka ticktack ambapo hupoteza muda ili kuongezewa muda wa bunge ambao maana yake ni kuzidi kuzichanga njuluku.
Pia nimegundua kuwa bi mkubwa wangu bingwa wa kunitusi hana haja ya kunijaza presha wakati kuna sehemu anaweza kutumia ujuzi huu na kutengeneza njuluku kama bi Makaidi  na wale wote walioingia na waume zao kama Magreth Sixx na wengine ambao leo siwataji. Hana haja ya kufanya utapeli kuwa ni mganga wa kienyeji kama Kimdunge Ngumbaru Mwehu. Mitusi na mipasho yake inatosha kuingiza mamilioni ya madafu au vipi? Hivyo kwa sifa hii ya ubingwa wa mipasho lazima naye a-qualify kujiunga na bunge hili la ulaji.
 Ili kuhakikisha tunaongezewa muda wa kutengeza njuluku, napanga kuanzisha taasisi itakayoitwa UKULA yaani Umoja wa Kutetea Ulaji Laini ili kupambana na ile inayoitwa UKAWA ya wakosoaji na wapingaji. Katika kutetea hoja zangu nitahakikisha narudia yale aliyosema Njaa Kaya wakati wa kuvuruga Bunge husika kulikoitwa kulifungua. Nitakariri maneno yake kama ngonjera ili ajue nami namzimia.
Ukiona imezidi imepungua una-Jonikomba kwa kutishia kuingia mwituni kupigania ndoto zako hata kama ni za alinacha au vipi? Kwa wasiojua maana ya kujonikomba ni kwamba unachimba mkwara wa kishamba kuwa kama utakalo halitapitishwa basi unaingia mwituni kufanya kitu mbaya ili kuangusha sirikali. Wapuuzi hawa wanaobwata hovyo hovyo wana bahati. Ingekuwa wakati wa mzee Mchonga ukabwata hivi si ungesahaulikia na kuozea lupango. Shukuruni mnaendeshwa na wababaishaji wenzenu wanaochekeachekea upuuzi.
Kwa vile utwawala wa sasa unashabikia upuuzi kama kujonikomba kulukuvi hata kunjaakaya basi nami nitahakikisha nacheza the same tune to make njuluku au vipi? Lazima nipange mitusi mizito ya kumporomoshea pilato Joseph Waryuba nionekane mzalendo hata kama ukweli mimi ni zandiki na msaka tonge.
Ngoja nikaandae misokoto ya bangi na gongo vya kwenda kutumia mjengoni kama alivyosema Jobless Nduguy kuwa kuna waishimiwa wanakula ndumu na kunusu bwibwi.
Chanzo: Nipashe  Mei 3, 2014.

No comments: