The Chant of Savant

Sunday 26 October 2014

Mlevi kuanzisha IpTL yake


          Baada ya kugundua wadanganyika wanavyodanganyika na kuibiwa kirahisi kwa kusalitiwa na wakubwa zao, nami nasukuti kuanzisha Independent perfidy Thuggery Limited aka Interdependent papa andTumbili Limited (IpTL) ambapo nitakuwa nawakamua walevi njuluku kwa kudai kuwa nitawauzia bangi na gongo kwa bei mchekea na wakati mwingine kuwapa dezo wakati ni mkenge. Najua nitashinda hasa ikizingatiwa kuwa mimi sitaiba njuluku ya wafadhili kama wao bali ya walevi. Hivyo, sina hofu ya wafadhili kusimamisha misaada yao ili kunikomoa. Kwanza, walevi si ombaomba na hawategemei misaada ya wafadhili. Nani anaweza kuwafadhili fyatu wasioogopa mtu? Laiti kaya nzima ingekuwa na akili na tabia kama zetu huenda haya manyang’au yangeishaGaddafiwa kama si kuMabutuiwa.
Naamini walevi watauingia mkenge kirahisi. Kwani najua hawatajali hasa ikizingatiwa kuwa kwao bangi na ulabu vinaruhusiwa kama haki za walevi tofauti huku kinachoruhusiwa ni ulevi wa madaraka na si wa gongo wala bangi. Hivi wavuta bangi na walevi na wezi wakubwa kama hawa wa IPtL nani wabaya kama tutakuwa wakweli? Hivi walevi wa bangi na gongo wanamwibia au kumuumiza nani zaidi ya wao wenyewe na saa nyingine na bi wakubwa zao? Je hawa wa madaraka wanaumiza na kuaibisha wangapi? Hivi kweli si aibu kwa kaya iliyojaliwa kila aina ya raslimali na aslimali kuombaomba utadhani tuliumbiwa jangwani! Hata jamaa zangu wamanga wa jangwani hawaombi. Wanajua jinsi ya kutumia wese lao. Nasikia siri kubwa ya mafanikio ya wamanga ni kutotoa uraia wao kama njugu kama ilivyo Danganyika ambayo wageni hasa matapeli wameigeuza danguro na shamba la bibi.
Hebu jiulize tunatoa uraia kwa magabacholi wangapi kwa mwaka? Hivi unaweza kwenda kwao ukapewa uraia? Je tumejaza wakimbizi wa kiuchumi wangapi? Mitaa ya Sinza mnanipata ambapo najua kuna matapeli kibao wa Kinigeria waliowaingiza mjini mabinti wa kibongo kwa ushamba wao wa kushobokea wageni wasijue ni apeche alolo kuliko wao. Je tunao wakenya wangapi ambao wanakimbia njaa na dhiki kwao wanaokuja kuchukua ajira za wadaganyika kwa kisingizio cha kujua ung’eng’e wakati hawajui kitu? Wangeujua wangesomesha vitegemezi vyao kwa M7? Hayo tuyaache.
           Kama nitafanikiwa kuanzisha IpTL basi mchongo wangu wa kwanza nitauita Escrew yaani Endelea kuwa-screw walevi hadi wakome. Nitakula bila kunawa tena kwa miguu na mikono baada ya kuangukia hii njuluku ya walevi.  Chini ya mchongo wa Esrew lazima nitawashirikisha mwanasheria mkuu wa walevi, waziri wao wa njuluku,  na wengine wanaoonyesha kushabikia ulaji wa kilafi wa mikono na miguu bila kunawa.
          Najua nikianzisha zali hili bei ya bangi na ulabu itapanda kiasi cha maisha ya walevi kuwa mabaya kama ilivyo nishati kwa wachovu ambao hata hivyo wameendelea kuliwa wakijiona wasifurukute. Hata hivyo, kuna haja ya kujali katika ulimwengu wa kulana kama samaki? Kwa vile nina jamaa yangu bonge la tapeli aitwaye Jimmy RugeSingasinga, lazima nimpe kibarua ya cha kuwaingiza walevi mkenge mchana kweupe. Ila kwa walevi walivyo fyatu kama sitafanikisha dili hili bila kuacha nyayo kama wale wapumbavu na waroho wakigundua watanichoma moto kama kibaka. Maana wanavyochukia mibaka bila shaka wanaweza hata kugawana nyama yangu na kuwapa mbwa kama siyo fisi.
          Kwa vile siku hizi bangi na ulabu vinaonekana kupungua, nitawafunga kamba kwamba nina mpango wa kufungua kiwanda cha kisasa cha kutengeneza ulabu na kile cha kusindika bangi na kugawa bure. Kwa vile walevi wanapenda sana vya dezo, watauingia mkenge wangu. Nitaita ahadi hii Maisha Safi kwa Walevi (MASAWA) ambayo kimsingi si maisha bora chochote bali kuwekana sawa ili walevi waliwe tu.
          Kwa vile nimesoma mchoro mzima wa IPtL kama ilivyoanzishwa akina Horse Kolimbaye,Kig-oma Milima, Saymon Mhaville, Ali Sahani ya Mwinyi, Ben Makapu Endelea Chenga, Abdi Kigodae, Dan son of Jonah, na majambawazi wengine wakubwa na wadogo waliowaingiza wadanganyika kwenye zali za IPtL inayozidi kuwanyonya na kuharibu maisha yao, nami nitafuata mbinu zote waliozotumia. Hata hivyo, nina shaka. Maana walevi pamoja na ulevi wao si mataahira kama wadanganyika wanaodanganywa na hata mafala na mataahira kama ilivyo. Ukiliangalia jitu kama Jimmy RugeSingasinga na jisura na akili yake mbaya unashangaa liliwezaje kuwaingiza mkenge? Ngoja niachane na sura za akina handsome and beautiful. Maana mtu anaweza akawa handsome lakini akaishia kuwa bogus upstairs na mwingine akawa ugly kuanzia roho akili hadi sura kama Dugong aka Dangerman Makapu. Hayo tuyaache.
          Tofauti na wadanganyika, mie sitaiba njuluku zaidi za walevi kwa kumtumia ponjoro wala gabacholi kama walivyofanya kwa kumtumia jambazi kibaraka wa akina Daniel arap Mwehu wa kule kaya ya manyang’au ambaye jamaa yangu hivi karibuni alinilalamikia kuwa wanajipenyeza Danganyika wakijifanya akina Mura wakati si kweli. Hawa jamaa kwa ulafi uchoyo na roho mbaya sina mfano. Nasikia baadhi ya vyombo vya umbea vinawalipa mshiko mkubwa huku wakiwa vihiyo na kuwapunja wadanganyika.Wachome wakitoe wakafakamie makande kwao. Hayo tuyaache.
          Nikishaanzisha IpTL naamini nitachanga njuluku kiasi cha kupata njuluku nyingi kuliko hata zile za EpA na Escrew ambazo nitazitumia kugombea urahisi na ulaji wa dezo ili kutanua ughaibuni na bi mkubwa na washirika zetu. Kwa vile walevi wamelewa sana kiasi cha kutojitambua, naamini watauingia mkenge sawa na huu wanaokaribia kubamizwa na akina Sam Sixx na Njaa Kaya.
          Nami nitashirikiana na walevi walio chini yangu ili kuhakikishia likibumburuka tunalindana kama wanavyofanya wao ambapo kila mwizi anajifanya hajui kitu wakati nyuma ya pazia unakuta kuwa wote ni kambale, wana sharubu au tuseme ni vyangu kwa vile wote wana magamba. Nani alidhani kuwa wale walevi wanaowakimbilia kushitakia uoza wao wameushiriki na saa nyingine wameoza kuliko hata hao tunaowaona mbele ya pazia?
          Kwa ufupi ni kwamba baada ya kugundua kuwa usaliti hasa wa kuwaibia wale waliokuamini unalipa nimeamua nijitajirishe kwa kutumia njuluku za walevi.
CHANZO: NIPASHE

No comments: