The Chant of Savant

Tuesday 23 December 2014

Mlevi amshauri Obama amheshimu dingi wetu

  
     Pamoja na mibangi na ulabu wangu, huwa ni mpenzi wa rais Brack Obama wa kwa Joji Kichaka. Namhuhusudu kwa jinsi alivyopenya ubaguzi wa kunuka kuanzia kule Furgson Missouri hadi New York ambako jamaa alikabwa na ndata hadi akanyotoka roho huku wakiendelea kumkamua zaidi.  Nahusudu jinsi alivyochipuka hadi akawa dingi wa kaya hii yenye nyodo na ukwasi wa kutisha japo unaanza kuyoyoyoma baada ya kujiingiza kwenye vita na ugaidi.
          Pamoja na kumhusudu huyu rais ambaye si rahisi kukingia kifua ufisadi na mambo ya hovyo kama wale niwajuao, juzi alifanya nianze kufikiria upya juu ya kuendelea kumshabikia, kumshobokea, kumpenda hadi nikwaza kumponda.
          Hakuna kitu ameniudhi hadi nikatamani nimnyotoe mtu roho kama kumtumia balozi wake kumtishia dingi wetu mpendwa na kipenzi cha watu akisema kuwa kama hatawashughulikia washikaji zake walio-screw walevi kidogo atamnyima njuluku.  Sifichi, wala kuomba msamaha. Obamiza aache kuingilia mambo yetu ya ndani hata kama hayakufurahishi.  Tuna namna yetu ya kufanya mambo yetu hata kama ni ya hovyo. Rejea jinsi hivi karibuni waishiwa wa upingaji na Chama twawala walivyokubaliana kumaliza kashfa ya escrew kwa kuwakaanga baadhi ya watuhumiwa huku wakiwanusuru wengine ili kuonyesha mshikamano na namna wanavyofanya mambo kivyao vyao.
          Tunamshauri Obamiza asiingilie mambo yetu. Anaonekana kukerwa na ulaji wetu utadhani ndiye mwenye kaya. Kama wenye kaya wanaupenda na kuuvumilia yamhusu nini? Tunamshauri asiwafundishe wachovu wetu wapenda amani ubishi kama wa wamarikani. Kwetu mkubwa hahojiwi wala kukosolewa hata kama anayefanya hivyo ni mkubwa mwenzake. Kumkosoa mkubwa ni kumkosea adabu na haivumiliki. Inakuwa nongwa hasa unapokosoa changuo la Mungu na walevi. We toa mshiko wa kuhomola wahomole na wa kuficha Uswizi wafiche. Uishie hapo. Usiwabughudi waheshimiwa walaji.
          Sisi si maskini. Kwani njuluku wanayolingia wafwadhili haiwezi kulingana na ile ya Richmond, EPA na sasa escrew au ile tunayozamisha kwenye uchakachuaji na bado tukaita mizengwe hii demokrasia kuonyesha jeuri yetu ya njuluku. Pili, ajue kuwa akija hapa kugombea huo urais hawezi kupata kwa vile hana jeuri ya mshiko ya kutembeza takrima ili watu wamkrimu ulaji kama hapa kwetu ambapo wasio na njuluku hawawezi kuwa viongozi.  Sisi yetu ni njuluku. Tufuje tusivuje inamuhusu nini? Yeye kazi yake ni kutoa nasi yetu kutumia tutakavyo hata kama ni kwa kuweka kwenye visiwa vya Jersey, Uswizi au Islands of Man. Akiendelea kutuletea za kuleta wengine watatoa. Tutakwenda zetu China Uarabuni hata kwa Putin na kuchukua njuluku na kutumia tutakavyo kwani zake?
          Namtaka wazi amheshimu dingi wetu mpendwa kipenzi cha walevi ambaye hawezi kumlazimisha eti awakamate watu tena washikaji zake ili wamchukie aache kuwa kipenzi chao. Hatutaki ukoloni wa kuendelea kufikiri kuwa mnaweza kuendelea kutuamuru hata jinsi ya kufuja sorry kula njuluku zetu. Zinakuwa zenu kabla hamjazitoa. Mkishazitoa ni zetu. Hata kama mnaona kama tunafanya ufisadi nyinyi unawahusu nini? Mnasema eti tunachezea raslimali zetu nyinyi zawahusu nini? Tumieni zenu vizuri si mtuache na mambo yetu. Hivi akitokea njemba akamwambia Obama aache silaha za nyuklia atakubaliana naye? Kama dharau hii itaendelea tutavunja uhusiano. Sisi ni kaya makini yenye kujua inachofanya hata kama kitaonekana hovyo kwenu. Dingi mstaafu Benny Mkaxx alisema kuwa uwekezaji hata uwe wa kichukuaji na kifisadi ndiyo njia pekee ya kuweza kuikomboa kaya. Hili halijabadilika. Tuacheni tufanye vitu vyetu.
          Tuombeni msamaha kwa kuingilia mambo yetu ya ndani. Mjengo umeishapitisha hukumu kuwa baadhi ya watuhumiwa wakaangwe ili kumaliza mambo, sasa wasi wasi ni nini? Kitendo cha kutaka kukamata wapendwa walaji kwa kuchukua vipesa vya ugolo kama vile ni magaidi wa Guantanamo ni cha kulaaniwa.
          Dingi wetu na chama chake ni wasafi kama theruji. Ni wachapa kazi na wapenda watu. Kuthibitisha alivyo mchapakazi, dingi wetu huwa hata halali nyumbani, hulala kwenye ndege akisafiri huku na kule kutafuta fedha ya kuendesha kaya yenye upendo mkubwa na majirani zake. Rejea taarifa kuwa kwa sasa majirani wasio na inchi ya udongo wenye tanzanite wanauza hii kitu kwa wingi kuliko Bongolalaland. Pia dingi wetu huwa hapendi kuona ngurumbili wakiteseka. Rejea wauza bwimbwi wanavyowapa bwimbwi wabwiaji ili wapate raha. Alishasema raha jipe mwenyewe. Kaya yetu ni ya kupeana raha. Ukinunua bwimbwi unabwia bila noma hata mkijazana mitaani hakuna wa kuwaghushi lau mmuonyesha mnapopata kitu hii. Wengi wanasahau kuwa dingi wetu ni zao la awamu ya ruksa ambapo kila kitu ni halali kiwe haramu au jinai. Hapa unachopaswa kufanya ni kuchukua za wenzako na kuchanganya na zako na kufanya mambo au vipi?
          Uongozi wa dingi yetu umefanya kaya yetu ipendwe na wawekezaji kama vile Harbinger Sweat Sing na Jimmy Rugemalayer ambao wameifanya nchi yetu iwe maarufu hadi kumkera Obama. Uwekezaji wetu ni wa ukarimu ambapo mwekezaji anaruhusiwa kuchukua atakavyo huku akisamehewe kodi kila baada ya miaka mitano kupitia kuruhusu kubadili jina la kampuni ili afaidi misamaha ya kodi maisha. Obama anaweza ukarimu huu? Athubutu wamtoe mkuku White House.

          Tumalizie kwa kumshauri aachie hizo njuluku alizozuia. Kuendelea kuzibania ni kinyume cha haki za ngurumbili. Wewe kata pochi. Mambo ya zinaliwa yanakuhusu nini wakati kazi ya njuluku ni kuliwa? Kama wanaoliwa wanafurahia kuliwa, pilipili usiyoila yakuwashani?  Isitoshe, Obamiza na wafadhili wanadhani kelele zao zitazuia watu kupiga madili na kutajirika bi vu kwenye kaya ambako hata ukimkaba mtu hadharani ukampora na kuwa milionea hakuna wa kukuuliza bali kukuabudia? Dingi aliwahi kusema: Kelele za wapanganji hazimnyimi usingizi mwenye ubavu wa mbwa. Nampa Obamiza wiki moja aje kwangu nimpangie lau dakika kumi aombe msamaha.
Nipashe Jumamosi

No comments: