The Chant of Savant

Tuesday 2 June 2015

Kijiwe chasherehekea kufunguliwa kwa wagombea


Baada ya kamati kuu ya mizengwe ya chama cha mizengwe kufanya mizengwe yake: kusema imewafungulia wataka urahis wake, Kijiwe kimepokea habari hizi kwa hisia tofauti mojawapo ikiwa ni kujiandaa kuwalia njuluku zao na kuwapiga chini.
Mchunguliaji analianzisha, “Waheshimiwa mmesikia mizingwe ya kufunguliana utadhani kulikuwa na mtu kifungoni? Hapa cha mno ni kufungua msimu wa kununuana na kuuzana ili ipatikane kura ya kula dezo. Lazima walete na kumwaga fedha zao na lazima ziliwe na lazima kura wanyimwe.”
 Mijjinga anakula mic, “Kwani walikuwa wamefungiwa au ni kutufunga kamba.  Mbona wengi wao walikuwa wakiendelea kupiga kampeni kupitia visingizio na sanaa mbali mbali? Waliofungwa hapa ni wapiga kura wasipokuwa makini wataula wa chuya kama kawa.”
Kapende anapoka mic, “Naona kama jamaa wanaanza kugeukana kwa kuogopa kupigwa chini. Wale tuliodhani kuwa walikuwa marafiki wa kweli kumbe walikuwa wameunganishwa na ulaji! Naona jamaa baada ya kuupata na kuufaidi ameamua kumtosa mwenzie japo alimtosa tangu zama za Richmonduli alipomuachia zigo lake alibebe peke yake. Ningekuwa mimi nisingekubali bali ningemwaga mtama lau kila mtu apate haki na stahiki yake.”
Mipawa anakatua mic, “Wewe unaongelea kuwa wanaweza kupigwa chini. Kwani hawatapigwa chini usawa huu? Wapigwe chini mara ngapi? We ngoja utawasikia. Cha mno hapa ni kuhakikisha kuwa hatukubali uchakachuaji na upuuzi mwingine.”
Anaendelea, “Pia nashauri wapinzani wajiandae kikamilifu kuwahamasisha wachovu kulinda kura zao ambazo licha ya kuwa haki yao ni mstakabali wao.”
Mbwamwitu hajivungi, anakatua mic, “Kwa hali ilivyo lazima kiumane. Hamkusikia Njaa Kaya akiwaonya kuwa waache kukalia mazoea ya uchakachuaji na kubebana wasijepigwa chini.”
“Yakhe mie siku watopigwa chini ntasherehekea ajuaye subhanna mwenyewe. Maana wanchosha hawa eti. Kila mwaka kila uchaguzi wao waiba na kudokoa tuuuu.” Mpemba anaukoleza.
“Tikubaiane. Siku hizi urais umegeuka urahis waahi. Hata wae wazinzi waiokamatwa kue Igunga na wake za watu eti nao wanataka kuugombea! Ingekuwa Tanga tingepiga mtu zongo waahi naapa.” Mgosi anaamua kulalama.
Mheshimiwa Bwege anatia guu, “Kwani wewe siku zote ulidhani urais si rahisi siyo? Kwa kaya isiyo na maadili bali madili hata kuku anaweza kuwa rahis na akatawala kwa kunya kila mahali bila kuguswa kwa vile anakuwa juu ya sheria.”
Anaendelea,“Mie naona heri ya kuku kwani atatoa mbolea kila mahali kuliko fisi na mchwa wanaoguguna kila kitu kam alivyo kwa sasa.”
Msomi Mkatatamaa anaingia kwa jam,“Jamani tuache utani. Urais ulikuwa wakati wa mzee Mchonga. Lakini baada ya wale aliowakataa kuukwaa huoni umegeuka ufanyabiashara na ulaji wa dezo? Tangu ilipotolewa ruxa ya kuiba na kufisidi kwa kadri mja atakavyo, urais wa kaya yetu uligeuka ujambazi wa mchana kusema ule ukweli.”
Mzee Maneno anakwanyua mic, “Usemayo ni kweli Msomi. Ndiyo maana kila fisadi anaugombea na kuutaka hata bila ya kujipima kama wachovu wanamtaka. Kimsingi, hapa kinachofanyika ni kuchagua walaji watakaokuja kutula.”
Mgosi hataki kupitwa, “Tafadhai futa kaui yako. Eti tinachagua watu wa kuja kutula. Haiwi mtu kama kuiwa utaiwa wewe si Mgosi.”
Mzee Maneno anajibu, “Mgosi ogopa sana kula. Mbona veve kula nyingine? Kama veve kula nyingine haiko baya kuliwa kidogo dugu yangu.”
Msomi anarejea tena, “Mimi nadhani mambo ya kuliwa tuachane nayo na kupanga jinsi ya kula fedha za mafisi na mafisadi wanaojifanya wanatupenda kwa sasa ili wapate kura yetu ya kula halafu watubamize mkenge. Hapa tegemea ahadi nyingi nono na nzito kama utajiri kwa wote, elimu kwa wote, vijana kwanza, akina mama kwanza na upuuzi mwingine. Hukumsikia yule kidhabu akisema eti atawekeza kwenye elimu kwanza na si kilimo utadhani anakula makaratasi? Ama kweli wanajua kututenda utadhani hatuna akili kama wao!”
Sofia Lion aka Kanungaembe anaamua kutia guu, “Hivi mnataka mliwe mara ngapi? Mtake msitake mtaliwa tu. Hakuna cha dezo. Hata hiyo njuluku mnayopanga kula lazima mlipie kwa mlango wa nyuma.”
“Sofi chunga hiyo lugha. Eti tutalipa kwa mlango wa nyuma, upi huo kama si matusi ya nguoni?”
“Mtajaza wenyewe, halo halo! Mtaipata pale itakapojibu baada ya matokeo ya kura kutangazwa na mkajikuta mmegaragazwa kama mende.” Sofia anakandia zaidi.
Kanji naye hajivungi, “Kama veve kula vatu nyingine nave taliwa tu. Tindo ya sasa ni kula na kulipa dugu yangu. Hapana ogopa liwa hii kitu dogo tu.”
Kama kuiwa diii basi iwa wewe si Mgosi. Tena misitake kunipandisha hasia nkapiga mtu zongo hapa hapa kijiweni ohoooo! Unadhani ninatania. Nitakushusha shipa hapa hapa.”
“Tafadhari Gosi acha tisha mimi. Kama veve veza shusha shipa basi nenda shusha shipa ile naibia veve halafu nahonga veve juluku naibia veve.”
Msomi anarejea, “Tuache utani. Tukiendelea na utani tutafanyiwa kitu mbaya kama ilivyokuwa 2005. Hapa tupange mikakati ya kula njuluku ya mafisadi wataka urahis lakini kura tusiwape. Tutapewa kila aina za urongo na ahadi ili tuuvae mkenge. Hukumsikia habithi mmoja akidai eti anasisitiza elimu utadhani anaweza kuishi kwa kula vitabu. Hata mbuzi hawezi kuishi kwa karatasi bali majani. Elimu gani wanaweza kusimamia wakati wameendekeza kulindana kwenye kughushi huku wakizidi kuua elimu? Shame on them all.”

Kijiwe kikiwa kinanoga si likapita shumbwengu la Eddy Luwasha. Acha tulitoa mkuku!
Chanzo: Tanzania Daima 3, 2015.

No comments: