The Chant of Savant

Tuesday 14 July 2015

Kijiwe chapokea matokeo kwa hisia tofauti


          Baada ya bata kuwika kule Idodomya ambapo wale ambao hukutegemea wamepitishwa, Kijiwe kimepokea mzengwe huko kwa hisia tofauti. Kwa ujumla Kijiwe kilishangilia kuona baadhi ya manyangumi fisadi wakimwagwa maji mchana kweupe.
Mpemba ndiye anaanzisha mada. Anasema, “Mie kweli nimeamini kuwa kama watu wetu wataamua waweza kuondoa kaya kwenye makucha ya mafisadi. Maana ukiangalia jinsi walivogawanyika na mitandao yao, wapingaji wapaswa kukaa mkao wakula wallahi. Hata hivo, sikutegemea kama huyu Aminia Salimia Ali angeweza kupenyezwa. Ana nini zaidi ya kutuhadaa wazenjmbari tujione kama nasi tumepenyeza ntu?”
“Heri ya huyu manzi. Maana hujui anakula na nani. Hakuna aliyeniacha hoi kama Jan Makamabaye nadhani anawakilisha watoto wa vigogo,” anakamua Mijjinga huku akibwia kahawa yake.
Kapende anaamua kumchomekea, “Unashangaa hiki kitegemezi ambacho kimepitishwa ili kuwazuga vijana? Nadhani hapa kiama kimeamua kujijenga kwa ndani kwa kuwazuga wanachama wake.” Anabwia kahawa na kuendelea, “Hata huyu manzi mwingine Migiriro naye sioni kitu hapo zaidi ya ujinsia jinsia.”
Mipawa naye anakwanyua mic, “Hawa jamaa watakuwa wehu kweli kama watategemea kuwa jinsia inaweza kuwapatia rahis. Kama Marekani pamoja na kuwa huru kwa maelfu ya miaka haijawahi kuwa na rais atokanayo na ujinsia, tunaharakisha nini? Naungana na wanaodhani kuwa manzi na vitegemezi wamepitishwa ili kuzuga makundi ya akina mama na vijana. Hata hivyo, kwa Janiwari wamenoa. Maana hawakillishi vijana bali vitegemezi vya vigogo.”
Msomi anapoka mic, “Kimsingi, mie naona wote walioletwa hawana lolote hata kama wapo wenye nafuu. Huwezi kuvaa kanzu chafu ukaswalisha ati. Mfano chinga kama Maembe ana nini zaidi ya ukaribu wake na Njaa Kaya na uhasama wa taifa? Angalau  Makufuli si haba ni mchapakazi japo ni shehe mwenye udhu lakini mwenye kanzu lililojaa najisi.”
Mheshimiwa Bwege anatia buti, “Mimi nilikuwa naomba wampitishe fisadi wao Eddy Luwasha ili wapingaji wazoe urahis kirahisi rahisi au siyo.”
Msomi anakwanyua mic tena, “Mzee ulikuwa umekosea. Suppose ungefanyika uchakachuaji akapita si wengi tungehama kaya?”
Kabla ya Msomi kuendelea, Mchunguliaji anaamua kutia timu, “Mie kama angepitishwa ningejinyotoa roho au kuhama kaya. Heri angepitishwa jaji Agus.”
Mzee Maneno anaamua kukatua mic, “Unakumbuka nilisema kuwa jaji Agus wasingempa hata kama ni mja safi. Nani anataka mlevi safi jaji na mwanajeshi ili awafanyie kitu mbaya?”
Mpemba anarejea tena na kuronga, “Hakuna kitu kilichonifurahisha wallahi kama Suhanna kupiga mafisadi laana hadi wakatembeza nshiko wasijue wengi wajaisha kwa presha.”
Mijjinga anadakia, “Ami umenikumbusha mzee Kimdunge Mwehu. Sijua ataiweka wapi sura yake. Mimi natabiri kifo cha Luwasha hasa baada ya kumwaga njuluku asiambulie hata tano bora.”
Msomi anarejea, “Mimi nina wasi wasi na mfumo wetu wa elimu. Inakuwaje kihiyo kama Joseph Makamba aweze kujipenyeza kwenye kigwena na kupitisha kitegemezi chake wakati wasomi waliokubuhu wakiishia kutoona mbali au ni kwa vile kaya hii ni ya vihiyo ukiondoa sisi Kijiwe? Maana unashangaa kuwaacha wabukuzi kama profesa Mark Mwando au nuclear physicist kama Dk Bilar unakumbatia wasanii kama Maembe Makambale na Aminia!”
Mijjinga anajibu haraka, “Ulitegemea nini toka kwa wachovu wanaotegemea kughushi badala ya kupiga mabuku?”
Sofia Lion aka Kanungaembe anakula mic, “Kwanza sikubaliani na uamuzi wa kumtupa mheshimiwa Luwasha kipenzi cha wengi. Hata kama mheshimiwa hakufanikiwa bado mshikamano wa chama uko pale pale. Asiyekubali kushindwa si mshindani. Nampongeza sana.”
“Nenda kampongeze nyumbani kwake uone kama mkewe hatakutia ngeu,” anachomekea Mbwamwitu.
Kanji naye kapata upenyo, “Sasa fedha yote namwaga na vatu nakula narudisha wipi? Ile bana iko roho juli sana. Nasaidia chovu sana. Kama nakuwa rahis kaye veza piga hatua na kuwa tajir kama nasema yeye Edi.”
Kapende anachomekea haraka haraka, “Hakuna cha roho nzuri wala kusaidia wachovu. Baada ya kumwagwa maji utaona kama ataendelea na huo ukarimu wa msimu. Kwa vile amekosa alichokuwa akikisaka, kama siyo kurejesha namba kwa shinikizo la roho na moyo atawachukia walaji na kuwaogopa kama ukoma. Kwani alidhani atawatumia asijue walimtumia na kumlia vyake.”
Mipawa anajibu kwa hasira, “Hafi ngurumbili hasa ikizingatiwa kuwa njuluku aliyokuwa akimwaga hakuitolea jasho. Hivyo, Bwana ametoa Bwana ametwaa.”
Mgosi Machungi ambaye leo alichelewa anaamua kutia buti, “Shikubai huu mchezo tinaofanyiwa. Kama wapiga kua watakuwa makini hata hawa jamaa wangeeta maaika angeshindwa kiahisi na wapingaji kama watajipanga vizui.”
Mijjinga anakamua mic tena, “Kama Eddy angesikiliza ushauri wa akina mzee Mpayukaji angeokoa lau njuluku zake. Badala yake alipuuzia alipoambiwa hatoboi. Akawa anawachukia wajumbe badala ya kuangalia uzito wa ujumbe.”
“Kidume Mpayukaji ni mtume aliyesalia hasa kwa wachovu,” anachomekea Mchunguliaji huku akichukua gazeti toka mezani kwangu.
Kijiwe kikiwa kinanoga si ukaja msafara wa wasanii wakienda kumuaga msanii mwenzao. Watakula mafi yao acha Makufuri muone kama lango la ikulu hamjawekewa kufuli msiende kumsanii rahis. Punde si punde ulifuatia msafara wa Luwasha ukienda zake kuomboleza kumegwa na kufishwa kwa ndoto zake za kuilangua kaya kwa washitiri wake.
Chanzo: Tanzania Daima Julai 15, 2015.

No comments: