The Chant of Savant

Tuesday 18 August 2015

Kijiwe chashangaa madaktari wa ndondi

  • The Honourable Dr. Titus Kamani Mlengeya
          Baada ya daktari mmoja mwenye kutia shaka alivyopata udaktari wake kutembeza masumbwi baada ya kubwagwa kwenye kura za kusaka ulaji, kijiwe kimekaa kumdurusu na kutoa mapendekezo yake. Kijiwe kinaainisha chanzo cha tatizo na kutoa suluhu.
          Japo si kawaida yake kuanzisha mada hasa ikizingatiwa kuwa huwa anaingia na magazeti na kuyasoma huku akingoja wengine wawasili na kulianzisha, Msomi Mkatatamaa leo kavunja mwiko. Analianzisha, “Jamani mmeona aibu hii kwa wasomi na wanasiasa iliyotekea kule Busegu?”
          Kabla ya kuendelea Mbwamwitu anachomekea, “Unaongelea hii aibu ya Dokta wa kutia shaka Tito Kimani kumpiga Dokta feki mwingine Chengeni nini?”
          Msomi anajibu, “Haswa. Maana imetutia aibu sisi wasomi. Laiti hii aibu ingeishia kwa wanasiasa badala ya wasomi nisingehuzunika.”
Kabla ya kuendelea Kapende anakula mic, “Ulitegemea nini baada ya kughushi na kutegemea shahada hasa udaktari wa kuzawadiwa kuhalalishwa kwa kila kihiyo? Kwanza nina wasi wasi hata kama huyu jamaa si wa kuzamia. Maana Kimani ni majina ya jamaa zetu wa kaya ya Nyayo.”
          Mijjinga hangoji. Anapoka mic na kusema, “Wewe unaongelea hii ya kushikana mikono kwa waghushi hawa! Mie hakuna kituko na kashfa iliniacha hoi kama yule mgushi mwingine anajiita dokta Didie Makalio naye eti kushinda kugombea jimbo la Ubungoni!”
          Mipawa anadandia, “Usipate ndugu yangu. Yuke tapeli laiti angeendelea na huo Umeyaa wake. Unadhani anaweza kumbwaga bwana mdogo Joni Mnyikani? Thubutu. Atapigwa chini. Tena nina mpango wa kumpelekea Joni taarifa nyeti za ufisadi za fisadi huyu na tapeli wa kutupwa.”
          Msomi anarejea, “Mnafahamu? Sijafahamu inakuwaje mtu anayeitwa msomi tena mwenye PhD kujiingiza kwenye mambo ambayo hata akina Tyson hawayafanyi pamoja na kuwa mabondia tena wa kupigiwa mfano!”
          Mheshimiwa Bwege anaamua kutia daruga, “Mheshimiwa Msomi acha nikupe somo hata kama wewe u msomi kuliko mimi. Kama ulikuwa hujui sasa elewa. Wakati mwingine usomi wa mtu especially anapokuwa ameungaunga na kughushi kama huyu, hauondoi upumbavu wake. Unadhani wanaosaini mikataba kibao ya kijambazi na kutumiwa na vihiyo kama Jimmy Rugemalayer na Singasinga wengine si ni wasomi wa kweli lakini ambao hawakuelimika.”
          Mgosi Machungi anamsapoti mheshimwa Bwege. Anaramba mic, “Sasa tinaongea nini? Hatijui kuwa mkuu wa Maekani hana PhD akini kaya yake ni kigogo kuliko yenu yenye mkuu mwenye PhD?”
          “Yakhe acha utani tena usinchefue. Sie Zenj tulikuwa na Daktari feki huyu akajipachika ukamandoo. Tuulize alifanyani zaidi ya kuzaa mafisadi kama akina Ladhaaa? Usemayo n kweli. Mtu aweza poteza muda shuleni asielimike na akielimika upumbavu wake usintoke wallahi.”
          Sofia Lion aka Kanungaemba kashikwa pabaya. Anakula mic, “Hivi watu wengine bila kumtaja mheshimiwa rahis hawawezi kulala? Sasa ulinganishaji wa Obamiza na mkuu unaingiaje wakati lile ni taifa kubwa ulimwenguni? Mie nadhani kama tunatenda haki tumchambue huyu Daktari Bondia kama mtu binafsi badala ya taaluma yake.”
          “Hata kama sina tabia ya kukuchomekea, acha leo nikuchomekee.” Msomi anasema. Kabla ya kuendelea Mbwamwitu anadakia, “Eti umfanye nini dada Sofi Msomi?”
           Msomi anagundua kosa lake katika matumizi ya lugha. Anajibu, “Namaanisha kudakia siyo kama unavyodhani wewe.”
           Kabla ya kuendelea Sofia anajibu, “Unadhani Msomi ni mpuuzi? Hata akiamua kunichomekea wewe yahuhusu au kukuuma nini?”
          Msomi anatikisa kichwa huku akishindwa kujizuia kucheka. Anatoa leso mfukoni na kujifuta machozi na kuendelea, “Jamani tuelewane. I am serious. I mean kudakia siyo vinginevyo. Anyways, tuendelee na mada. Kama da Sofi alivyosema ni vizuri kujadili mtu badala ya taaluma yake ingawa ni vigumu kumtenganisha mtu na taaluma yake kama kweli ni mwanataaluma. Nadhani alichoonyesha huyu daktari wa masumbwi ni ujinga usio wa kawaida. Hatai hivyo, angeshindwa nini kufanya hivyo wakati kughushi kumehalalishwa kayani? Wako wapi akina Mery Nyagu, Dodorus Kamala, Emmy Nchimvi, Diddie Makalio, Makorongo Muhanga, Adimu Milima ya Kigoma, Saaada Mkuyati na wengine walioghushi lakin rahis akawakingia kifua?”
          Kanji naye anaamua kula mic, “Mimi dhani sasa ghushi iko halali. Kama nataka leseni nagushi. Kama nataka itwa dokta lazima gusi. Kama nataka kuwa rahis lazima honga na gusi kula. Sasa kama kuba na toto yao vote nagusi nani hapana gusi dugu yangu? Sauri yako kana nakataa gusi tagusi veve.”
          Mijjinga anarejea, “Nadhani kuna kitu hamjui kuhusiana na huyu jamaa. Kama alivyowahi kueleza spika wao Jobless Nduguy, hawa jamaa wakati mwingine wanakata jani kiasi cha kuwabangua na kujivua nguo hadharani. Sababu nyingine licha ya jani ni ile hali ya kuwekeza sana kwenye siasa hadi wengine wanauza majumba au kuchukua mikopo ili kupata ulaji wa dezo na kujilipa. Usishangae wengine wanakijitundika kitanzi baada ya kubwagwa kutokana na kuwekeza sana kwenye mchezo huu mchafu.”
          “Hapo nimekuelewa ndugu yangu. Si bure lazima kuwe na kitu nyuma ya pazia.” Msomi anasema.
          Mbwamwitu naye anasema, “Hata mimi nimekupata vizuri sasa.”
Mijjinga huku akitabasamu anauliza, “Umeridhika sasa?”

          Kijiwe kikiwa kinanoga si akapita Kimani na marafiki zake. Acha tumtoe mkuku! Asindwe na anyong’onyee.
Chanzo: Tanzania Daima Agosti 19, 2015.

No comments: