The Chant of Savant

Wednesday 7 September 2016

Kijiwe chamstua dokta Kanywaji asiambukizwe majipu


 
            Juzi Mgoshi Machungi aliibahatika kuhudhuria mapokezi ya mkiti mpya wa Chama Cha Majipu, sorry Magamba, sorry, Mapandikizi (CCM) ambapo mkuu wake mpya alikuwa akirejea mjini baada ya kuizulu kaya lau kuonyesha makali na makucha yake ukiachia mbali kueleza mipango yake kwa wachovu.  Mgoshi alimfagilia sana munene kwa kuweka mambo hadharani kuwa chama chake ni bonge ya genge la mafisadi ambalo–licha ya kumilki vitega uchumi kibao–bado linaombaomba kila unapokaribia uchakachuaji kama alivyosema.
            Mgoshi analianzisha, “mmesikia mkuu aivosema kuwa chama chake ni genge la mafwisadi? Hakika waiosimamia uchafu na ufisadi huu ni majipu yanayomzunguka dokta Joni Kanywaji Makufui. Hivyo, anapswa kutahadhai yasimuambukize majipu kama siyo kumdhuu tokana na kugusa ulaji wao wa dezo.  Anapaswa kutumia hekima ya Yesu kuwa watakaomuambukiza majipu ni wale anayekula nao meza moja.”
Kapende anakula mic, “munene huyu alifanya kazi nyeti kweli kweli kiasi cha kuwavutia baadhi ya wanakijiwe nikiwamo mimi. Pamoja na dokta Kanywaji kuniridhisha sina shaka na baadhi ya mambo hasa baada ya kuonyesha anachopanga kufanya.”
            Mipawa anamchomekea Kapende, “mie sikushangaa kuona analaumu uoza chamani mwake huku akiwakingia kifua waliousababisha na kuuacha ugeuke kansa na jipu la kunuka yaani wanene wastaafu. Hatuna haja ya kurudia; kila mchovu anajua munene alivyosema tena hadharani na kwa kinywa kipana bila tena kunywa kuwa atawalinda wastaafu kwa gharama yoyote bila kujali uoza na uovu walioutenda. Hapa aliniacha hoi kiasi cha kuanza kuona kama kinachoendelea ni mchezo wa sanaa ambapo wanaoshughulikiwa ni wadogo huku wanene wakiendelea kupeta.”
            Kanji anakula mic, “yeye nakuna veve. Naacha mimi hoi. Iko sangaa kwanini safisha jumbani toka nje badala ya vunguni? Hapana ona kitandani yake jaa hii yote natetea?”
            Msomi Mkatatamaa anachumpa na mic, “tokana na spidi yake ya roketi kwenye kushughulikia dagaa, wapo wanaohofia kuwa kitendo chake che kuendelea kuwa karibu na majipu manene ambayo anaonekana kutoshughulikia, kunaweza kumwambukiza daktari mwenyewe majipu kiasi cha kuwa mgonjwa a majipu au jipu. Hili halihitaji shahada kwenye elimu ya siasa. Ukitaka kujua namna uambukizo huu wa hatari unavyoweza kufanyika–mbali na majipu staafu yalomzunguka daktari–tazama, majipu yaliyomzunguka. Hapa hatujaongelea mikashfa ya kunuka kama UdA, Escrew, SUKITA na mengine mengi ambayo yaliwahusisha baadhi ya makamanda wanaounda timu ya utumbuaji wakati wao ni majibu yanayonuka.”
            Mheimiwa Bwege anapoka mic na kusema, “dawa na usalama kwa dokta kuepuka majipu ni kuhakikisha anavaa glovu wakati wa kuyatumbua na kuhakikisha kuwa hayamkaribii popote alipo. Kwani yeye hafanyi kazi ya utume kama alivyosema Yesu kuwa alikuja kwa ajili ya wenye dhambi; hivyo, alikula nao. Dokta hapaswi kula na wagonjwa bali kuwatumbua majipu.”
            Mgoshi anamchomekea Msomi, “ngoja nikuchomekee ushahidi kidogo; hivi Bii Ukuuuviii aiyetuhumiwa kughushi si jipu kwei? Sijui majipu kama haya yanaweza kusaidia nini katika kutumbua mengine? Hata ukiangaia hicho chama chenyewe unashangaa. Kwani, waiokifinya kuwa jipu ni nani kama siyo hao hao wanaoimba sifa za dokta mtumbua majipu wasijue wao ndiyo majipu yenyewe. Sijui kama Andaaman Kinamna pale chamani si jipu. Maana, madudu yote yaiyokitafuna chama hadi kikafikia hata kutaka kumeguka yaifanyika chini yake na afiki yake aiyemteua baada ya kumpigia debe na kuukwaa ukuu aiotumia kama kijiko kwake na marafiki na famiia yake kujitaiirisha kwa kuwaibia wachovu.  Hivi kwei Kinamna ana jipya gani wakati muda wote likaa kwenye chama amekijenga kifisadi badaa ya kukisafisha? Hata hivyo, angesafishaje wakati naye aikuwa akifanya vitu vyake kama vie kampuni ake kudaiwa kusairisha vipusa nje na asifanywe kitu kutokana na wakati ue kaya kuwa kwenye outpiot? Nadhani huyu hana tofauti na Ombeeni Sifui aiyekuwa pale ikuu akipiga dii hadi dokta Kanywaji aipomtumbua. Kaka tumbua na huyu Kinamna kwani sifa zake zina namna.”
Mijjinga anakula mic, “hakuna aliponiacha hoi dokta kama kugusia namna chama kilivyo na mali nyingi kilichoiba kwa wachovu ila hazina faida kwa yeyote isipokuwa mafisadi wenye vyeo chamani. Hivi chama hiki nacho si jipu kweli? Kwanini kinusurike wakati kilinyakua ardhi ya umma wa walevi na kujilimbikizia kinyume cha sheria?”
            Kabla ya kuendelea Sofia Lion aka Kanungaembe anamchomekea, “ajabu ya maajabu, chama kile kile eti hakikuruhusu watu wajimilkishe maeneo makubwa ya ardhi kwa vile ni ukabaila wakati chenyewe ni chama kabaila?  Kuna haja ya wachovu kuanza kujiandaa kisaikolojia kulikabili hili genge na kutaka lirejeshe ardhi mali zao. Pia watamke wazi kuwa sera zake ni ubwanyenye na ukabaila lakini si vinginevyo. Huwezi ukamwaga nyama na mifupa ukabaki na mchuzi ukasema hujali nyama ya kile ulichomwaga. Ukabaila–tena wa kunyakua viwanja vya umma–ni unyama na jinai hasa kwenye kaya inayojinakidi kutenda haki na usawa kwa wote.”
            Leo wachangiaji wengi wamechonga sana kiasi cha kuwanyima wengine nafasi. Hata hivyo, tunachojali ni mipwenti. Naona yule ndege anacheka huku akitikisa kichwa na kushangaa!
Chanzo: Tanzania Daima Jumatano leo.
 

No comments: